Orengo ataka polisi kuachilia huru wandani wake waliokamatwa
GAVANA wa Siaya, James Orengo ameshinikiza kuachiliwa huru kwa baadhi ya wasaidizi wake na wafanyakazi wa serikali yake aliodai walikamatwa Jumamosi, Machi 7, 2026, siku moja kabla ya ziara ya Rais William Ruto katika kaunti hiyo.
Kupitia ujumbe kwenye akaunti yake ya mtandao wa X siku hiyo, Bw Orengo alidai kuwa watu hao walikamatwa Siaya na Nairobi saa za jioni na kuzuiliwa na polisi, akitaja kitendo hicho kama ukiukaji wa katiba na misingi ya kidemokrasia.
“Jioni hii (Machi 7, 2026) wafanyakazi kadhaa wa serikali yangu walikamatwa kiholela na polisi na kuzuiliwa Siaya na Nairobi kuhusiana na ziara ya rais Siaya Jumapili, Machi 8, 2026. Vitendo vibovu kama hivi vya polisi havina nafasi chini ya Katiba ya sasa inayoheshimu demokrasia. Nataka waachiliwe huru mara moja,” Bw Orengo akaeleza, bila kutaja majina ya watu hao aliodai walikamatwa na polisi.
Rais Ruto anazuru Siaya mnamo Jumapili kuhudhuria sherehe ya kutoa shukrani kufuatia kuteuliwa kwa Katiba wa Wizara anayesimamia Huduma za Matibabu Dkt Ouma Oluga, katika Shule ya Msingi ya Okela, Uyoma, eneo bunge la Rarieda.
Rais anazuru Siaya wakati ambapo migawanyiko na uhasama inashuhudiwa ndani ya chama cha ODM na kufuatia kuibuka kwa mirengo miwili ya “Linda Ground” na “Linda Mwananchi”.
Bw Orengo anaegemea mrengo wa Linda Mwananchi unaoongozwa na Katibu Mkuu anayepigwa vita Edwin Sifuna na unaopinga ushirikiano wa chama cha ODM na kile cha UDA chini ya serikali jumuishi.
Mrengo huo pia unapinga kuchaguliwa tena kwa Rais Ruto ukishikilia kuwa ODM itadhamini mgambea Uraia katika uchaguzi mkuu wa 2027.
Nao mrengo wa Linda Ground unaoongozwa na kiongozi wa chama Oburu Oginga na mwenyekiti Gladys Wanga, unaunga mkono ushirikiano wa vyama hivyo viwili huku ukirindima “injili” ya kuchaguliwa tena kwa Dkt Ruto katika uchaguzi mkuu ujao.