Habari

‘Picha ya Bikira Maria’ kwenye ukuta jikoni yaibua gumzo Kisii

Na WYCLIFFE NYABERI September 7th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

KATIKA vilima vya eneobunge la Bobasi, Kaunti ya Kisii, nyumba ndogo ya udongo ambayo kwa miaka mingi imekuwa ikitumika kama jikoni sasa imegeuka kuwa kivutio cha mamia ya waumini na wadadisi.

Ni katika kijiji cha Getare, Emenwa, ambako mkulima Mary Onsombi, ambaye ni Mkatoliki mcha Mungu, anasema aligundua picha inayofanana na Bikira Maria kwenye ukuta wa jikoni lake uliojaa weusi kutokana na moshi.

Kilichoanza kama kivuli hafifu Ijumaa kilikuwa kimevutia maelfu ya wanakijiji kufikia Jumapili. Watu walifika kutoka maeneo mbalimbali, wakiwemo wahudumu wa bodaboda, wanafunzi na wahubiri wa madhehebu tofauti, wote wakitaka kujionea kile wanachokirejelea kama “Bikira Maria”.

Jirani yake, Gladys Nyandika, alisema Bi Onsombi aliona picha hiyo alipokuwa ameketi karibu na jiko lake.

“Alifikiri ni moshi. Alichukua kipande cha kitambaa na kujaribu kuifuta. Kadri alivyoifuta, ndivyo ilivyozidi kudhihirika. Alisema picha hiyo ilifanana kabisa na sanamu ya ‘Bikira Maria’ aliye kanisani kwao,” alisema.

Jikoni humo hakuna jambo la kipekee. Kuna kuta za udongo zilizotiwa weusi na moshi wa kuni, jiko la mawe matatu na sufuria chache zilizoning’inizwa kwenye misumari.

Lakini kwenye ukuta wa kaskazini, karibu futi tatu kutoka chini na eneo ambalo Bi Onsombi hupiga magoti anapopika, kuna umbo la kijivu-nyeupe lenye urefu wa takriban inchi 18.

Kwa waumini, umbo hilo linafanana na mwanamke aliyevaa vazi refu na kufunika kichwa, huku mikono ikiwa kama yule anayeomba. Kwa wenye mashaka, huenda ni muundo uliotokana na moshi wa miaka mingi, maji kupenya ukutani na udongo kuchubuka.

Jikoni hiyo sasa imegeuka kuwa mahali pa sala, huku watawa na waumini Wakatoliki wakisongamana ndani wakiwa na rozari mikononi.

“Mungu akiamua kujionyesha, lazima uje uone, iwe wewe ni Mkatoliki au la,” alisema mfuasi wa SDA aliyesafiri kutoka Nyamakoroto, Nyamira.
Diwani wa Masige Mashariki, Michael Motume, alikuwa miongoni mwa viongozi wa kwanza kutembelea boma hilo.

Alisema aliona picha isiyo ya kawaida iliyofanana na sanamu maarufu ya Bikira Maria ya Kanisa Katoliki, lakini akasema hana mamlaka ya kuthibitisha iwapo ni muujiza.

Kufikia Jumapili asubuhi, njia ya kuelekea kwa Onsombi ilikuwa imejaa watu.

Baadhi walipiga magoti na kusali, huku wengine wakipiga picha na video kwa TikTok. Wahudumu wa bodaboda nao walipata biashara nzuri, wakitoza Sh100 kwa safari kutoka Emenwa Centre hadi Getare.

Watawa waliofika eneo hilo hawakutoa maelezo mengi, lakini walionekana kuchukua picha na kuandika kumbukumbu, huenda kwa ajili ya kuwajulisha viongozi wa Kanisa Katoliki katika Dayosisi ya Kisii.

Kanisa Katoliki bado halijatoa taarifa kuhusu madai hayo ya muujiza. Vyanzo vya kanisa vilisema halikimbilii kuthibitisha madai kama hayo.

Mtaalamu mmoja wa kanisa alisema ripoti kama hizo zimewahi kutokea nchini, zikiwemo picha zinazoonekana kwenye miti na miamba, na nyingi baadaye kubainika kuwa matukio ya kawaida ya kimaumbile.