Habari

Rais Ruto asisitiza Kenya haitauza madini ghafi nje ya nchi

Na NA MANASE OTSIALO September 7th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

RAIS William Ruto amesema Serikali yake inaandaa sera itakayokomesha usafirishaji wa malighafi kutoka Kenya kwenda nje, huku kampuni zikihitajika kuwekeza nchini, kuongeza thamani ya madini na kuunda nafasi za kazi.
Akizungumza akiwa Kaunti ya Samburu, wakati wa hafla ya kutoa shukrani ya Katibu wa Ugatuzi, Michael Lenasalon, Rais Ruto alisema amechukua hatua binafsi kuhakikisha usafirishaji wa madini kutoka Magadi unakomeshwa.
Alisema sera hiyo itahusu rasilimali zote za nchi, zikiwemo mafuta, dhahabu na madini adimu.
“Kuanzia sasa, msimamo wetu wa kisera ni kwamba iwe ni soda ya Magadi, mafuta au madini yetu yote, ikiwemo dhahabu na madini adimu, tumeamua kwamba hatutasafirisha tena malighafi,” alisema.
Rais alisema Serikali itahakikisha madini yanachakatwa nchini ili kuongeza thamani na kutoa ajira kwa Wakenya.
Alisema pia Serikali inashirikiana na mfanyabiashara Aliko Dangote kuanzisha kiwanda cha kusafisha mafuta Lamu.
Aidha, alisema Serikali inashirikiana na wawekezaji wengine kuanzisha viwanda vya kusafisha dhahabu na kuchakata madini katika maeneo mbalimbali nchini.
“Itakuwa si busara kwa Serikali kusafirisha malighafi, kuunda ajira na kuongeza thamani katika nchi nyingine wakati tuna vijana wengi wanaohitaji ajira,” alisema.
Rais alisema alilazimika kwenda Kajiado kushughulikia mkataba wa awali wa uchimbaji, ambao alisema ulikuwa ukinufaisha zaidi kampuni kuliko Wakenya.
 Alisema mkataba huo, ambapo Kenya ilipata asilimia tano pekee huku asilimia 95 ya thamani ikitengenezwa nje ya nchi, umefutwa.
 “Hatuwezi kufuata malighafi zetu nje ya nchi na kununua bidhaa kwa bei ya juu huku vijana wetu wakikosa ajira,” alisema.
Rais alisema tenda mpya itatangazwa na kampuni zaidi zitaruhusiwa kuwekeza Kajiado.
Alisema Serikali haitaki kampuni moja pekee, bali inataka zaidi ya kampuni tano na hata 10 zitumie rasilimali hizo kuunda ajira na kuongeza thamani.
Jumamosi, Rais alitangaza kuwa mkataba wa uchimbaji wa Tata Chemicals, iliyojulikana zamani kama Magadi Soda, utatangazwa upya kupitia zabuni yenye ushindani.
Alisema mkataba huo ulikuwa wa kunyanyasa Kenya na hauwezi kuendelea.
Rais Ruto pia aliahidi kuhakikisha ushirikiano wa kisiasa kati ya UDA na ODM unaendelea hata baada ya uchaguzi wa 2027.
 Alishukuru ODM kwa kusaidia kupunguza joto la kisiasa nchini.