Ofisi 3 zinazohusishwa na Rais Ruto zafyonza Sh100 bilioni-ripoti
OFISI tatu zinazohusishwa na Rais William Ruto zilitumia Sh33 bilioni katika mwaka uliokamilika Juni 2026, kiwango cha juu zaidi kuwahi kutumiwa na ofisi za maafisa wakuu wa Serikali, kwa mujibu wa ripoti mpya ya Wizara ya Fedha.
Matumizi hayo ya ofisi za Rais William Ruto, Naibu Rais Kithure Kindiki na Mkuu wa Mawaziri Musalia Mudavadi yanafanya jumla ya fedha zilizotumiwa na ofisi hizo tangu Kenya Kwanza iingie madarakani mwaka 2022 kufikia Sh100.23 bilioni.
Kwa miaka minne, matumizi ya urais yamezidi Sh89.9 bilioni zilizotumiwa na mtangulizi wake, Uhuru Kenyatta, katika miaka 10 ya uongozi.
Ripoti ya Wizara ya Fedha kuhusu hali ya uchumi na bajeti ya mwaka wa kifedha 2025/26 inaonyesha Ikulu ilitumia Sh18.4 bilioni.
Katika miezi mitatu ya mwisho ya mwaka huo, Aprili hadi Juni 2026, Ikulu ilitumia Sh6.8 bilioni. Hii ni sawa na wastani wa Sh570 milioni kwa wiki au Sh81.3 milioni kila siku.
Katika kipindi hicho, Rais Ruto aliandaa shughuli mbalimbali katika Ikulu, huku maelfu ya watu wakifika katika hafla kadhaa.
Miongoni mwa waliomtembelea Ikulu ni wanachama wa Maendeleo ya Wanawake mnamo Aprili 1, 2026, pamoja na viongozi wa mashinani kutoka kaunti mbalimbali.
Mnamo Mei 11, Ikulu pia iliandaa karamu ya kitaifa kwa wajumbe wa Mkutano wa Africa Forward.
Ikulu imekuwa ikitumia kiasi kikubwa cha fedha tangu Rais Ruto aingie madarakani. Kati ya Julai 2022 na Juni 2026, ilitumia jumla ya Sh43 bilioni, sawa na asilimia 43 ya zaidi ya Sh100 bilioni zilizotumiwa na ofisi zilizo chini ya Urais.
Katika robo ya kwanza ya mwaka wa kifedha 2025/26, Ikulu ilitumia Sh4.56 bilioni. Kiasi hicho kilishuka hadi Sh3.17 bilioni katika robo ya pili, kabla ya kupanda hadi Sh3.85 bilioni katika robo iliyomalizika Machi 2026.
Katika robo ya mwisho, matumizi yalipanda kwa karibu theluthi mbili hadi Sh6.83 bilioni.
Kati ya Sh18.4 bilioni zilizotumiwa na Ikulu katika mwaka huo, Sh17.12 bilioni zilitumika katika shughuli za kawaida.
Fedha hizo ziligharamia mishahara ya wafanyakazi, mafuta ya magari ya viongozi, marupurupu na tiketi za ndege za maafisa wanaosafiri ndani na nje ya nchi, pamoja na chakula cha wageni.
Kwa mwaka huu wa kifedha, Ikulu imetengewa takriban Sh13.5 bilioni, ingawa kiasi hicho kinaweza kubadilika wakati wa marekebisho ya bajeti.
Ofisi ya Rais ilifuata Ikulu kwa matumizi ya Sh8 bilioni. Kati ya kiasi hicho, Sh6.68 bilioni zilitumika katika shughuli za kawaida.
Hii ni wastani wa Sh667.75 milioni kila mwezi au karibu Sh22 milioni kila siku.
Ofisi ya Naibu Rais Kindiki ilitumia Sh5.2 bilioni, huku Sh100 milioni pekee zikitumika kwa shughuli za maendeleo.
Kwa upande wake, Ofisi ya Mudavadi ilitumia Sh602 milioni, zote zikiwa za shughuli za kawaida.
Idara ya Serikali ya Masuala ya Bunge ilitumia Sh433 milioni, huku Idara ya Serikali ya Masuala ya Baraza la Mawaziri ikitumia Sh226 milioni.
Kwa jumla, matumizi ya ikulu, Ofisi ya Rais, Ofisi ya Naibu Rais na Ofisi ya Mkuu wa Mawaziri yalifikia asilimia 98 ya Sh32.9 bilioni zilizotumiwa na Urais.
Mwaka wa kifedha 2024/25, Urais ulitumia Sh21 bilioni, chini ya Sh22.8 bilioni zilizotumiwa mwaka uliotangulia na Sh23.3 bilioni zilizotumika katika mwaka wa kwanza wa serikali ya Rais Ruto, 2022/23.
Msemaji wa Ikulu Hussein Mohamed alisema matumizi yote yaliidhinishwa na wabunge.
Alisema ofisi zilizo chini ya urais hazitekelezi miradi moja kwa moja, bali zinahusika zaidi na sera, uratibu na kusaidia utekelezaji wa majukumu ya Rais na Naibu Rais.