Habari

Raila, Karua wachelea kutuma jumbe za risala hadharani kwa kifo cha Chebukati

Na CHARLES WASONGA February 21st, 2025 Kusoma ni dakika: 2

HUKU viongozi wakuu nchini wakituma risala za rambirambi kufuatia kifo cha Bw Chebukati, aliyekuwa mgombea wa urais wa muungano wa Azimio katika uchaguzi mkuu wa 2022 Raila Odinga na aliyekuwa mgombea mwenza wake Martha Karua walichelea kutuma jumbe zao.

Hata hivyo, kiongozi wa Wiper Kalonzo Musyoka, ambaye angeteuliwa kuwa Waziri Mkuu, iwapo Odinga angeshinda, alituma ujumbe mfupi kumwomboleza Bw Chebukati.

“Natuma rambirambi zangu kwa familia na marafiki wa aliyekuwa mwenyekiti wa IEBC Wafula Chebukati. Naiweka familia yake mawazoni na kwenye maombi wakati huu wa huzuni,” akasema kupitia akaunti yake ya mtandano wa kijamii wa X.

Kufikia sasa kumi jioni (4.00pm) Ijumaa, Februari 21, 2025, saa saba baada ya habari kuhusu kifo cha Bw Chebukati kutolewa rasmi, Bw Odinga hakuwa ametuma rambirambi zake wala kutuma ujumbe wa pole.

Uchunguzi wa Taifa Leo katika majukwa ya akaunti zake za mtandao ya kijamii, anayotumia kila mara haswa kutuma risala za kuomboleza vifo vya watu mashuhuri, ulibaini kuwa ujumbe wake wa mwisho ni kuhusu mkutano kati yake na Rais wa Burundi Evareriste Ndayishimiye mnamo Februari 12, 2025.

Bw Odinga alikutana naye jijini Bujumbura katika kampeni zake za mwisho za kuomba kura kuelekea uchaguzi wa uenyekiti wa Tume ya Umoja wa Afrika (AUC) ambao alishindwa.

Kwa upande wake Bi Karua, ujumbe wa mwisho kwenye akaunti yake ya X unahusu kujumuika kwake na raia wa kawaida wakifurahia kinywaji cha kahawa katika kibanda cha Sammy kituo cha kibiashara cha Githiga, eneo bunge la Gichugu, kaunti ya Kirinyaga.

Mnamo Agosti 15, 2022 marehemu Chebukati alimtangaza Rais William Ruto kama mshindi wa uchaguzi wa urais wa Agosti 9, matokeo yaliyopingwa na wawili hao kwa kuwasilisha kesi katika Mahakama ya Juu.

Hata hivyo, kesi yao ilitupiliwa mbali na Dkt Ruto akaapishwa kuwa Rais wa tano wa Kenya.

Aliyekuwa Naibu Rais Rigathi Gachagua pia alichelea kumwomboleza Bw Chebukati.

Ujumbe wa mwisho katika akaunti yake ya X ni kuhusu hafla ya kikanisa nyumbani kwake Wamunyoro alioongoza na mkewe Pasta Dorcas.