Habari

Ruto avunja kimya kuhusu kifo cha Albert Ojwang

Na BENSON MATHEKA June 11th, 2025 Kusoma ni dakika: 1

RAIS William Ruto ameagiza Huduma ya Kitaifa ya Polisi kuchukua hatua dhidi ya maafisa waliohusika na mauaji ya mwalimu na mwanablogu Albert Ojwang baada ya kukamatwa na maafisa wa usalama.

Katika taarifa iliyotolewa na Msemaji wa Ikulu, Hussein Mohamed, Rais William Ruto aliagiza kwa Huduma ya Kitaifa ya Polisi (kushirikiana kikamilifu na Mamlaka ya Kusimamia Utendakazi wa Polisi (IPOA) ili kufanikisha uchunguzi kamili kuhusu mazingira ya kifo cha Albert Ojwang akiwa kizuizini.

“Kwa hivyo naitaka Huduma ya Kitaifa ya Polisi kushirikiana kikamilifu na Mamlaka ya Kusimamia Utendakazi wa Polisi na kuchukua kila hatua inayohitajika kuwezesha uchunguzi wa haraka, wazi na wa kuaminika kuhusu kifo cha Ojwang,” alisema Rais Ruto.

Rais aliongeza kuwa taifa linaomboleza kifo cha kijana huyo, lakini akawaonya wananchi kutoharakisha kutoa matamshi yanayoweza kuhatarisha mchakato wa uchunguzi.

“Tunapomwomboleza marehemu, tuendelee kufuatilia kwa subira lakini kwa umakini maendeleo ya uchunguzi huu bila kutoa uamuzi mapema au kuhukumu kabla jambo ambalo linaweza kudhoofisha mchakato huu na matokeo yake.”

Aidha, Rais alisisitiza kuwa anasubiri taarifa kamili kutoka kwa mashirika husika kuhusu yaliyotokea na hatua zilizochukuliwa.

“Natarajia kwa dhati kwamba ukweli kuhusu yaliyompata Ojwang utadhihirika kwa wakati ufaao, na kwamba haki itatendeka.”

Rais alisema habari za kifo cha Ojwang zilimshtua kama mzazi mwingine yeyote akisema kinahuzunisha.

Alisema kazi ya polisi na kulinda Wakenya na mali yao na kufariki kwa mshukiwa akiwa mikononi mwao hakuwezi kuchukuliwa kwa urahisi.