Serikali yapanga kuongeza bei ya soda, juisi ili wananchi wadumishe afya bora
BEI ya vinywaji kama soda, juisi, na maziwa ya mtindi inatarajiwa kupanda iwapo Bunge la Taifa litapitisha pendekezo la kuanzisha Ushuru wa Uimarishaji Afya.
Mbunge wa Nandi Hills, Bw Bernard Kitur, ameomba Kamati ya Bunge kuhusu Fedha kuweka ushuru huo katika Mswada wa Fedha wa mwaka 2025 kama njia ya kupunguza matumizi ya vinywaji vyenye sukari nyingi, ambavyo vinachangia ongezeko la magonjwa kama unene, kisukari na maradhi mengine yasiyo ya kuambukiza (NCDs).
“Ushuru huu unalenga kupunguza matumizi ya sukari, kuhimiza utengenezaji wa bidhaa zenye afya zaidi, na kusaidia kufadhili kampeni za afya, mipango ya lishe shuleni, na miundombinu ya afya,” alisema Bw Kitur.
Mbunge huyo aliambia kamati hiyo kwamba ushuru huo utatozwa watengenezaji na waagizaji wa vinywaji vilivyo na sukari.
Alisema kipimo ni 4g/100ml kutotozwa ushuru ila gramu yoyote zaidi ya hapo itavutia ushuru huku watengenezaji wa humu nchini wakitozwa kwa kiwango cha Sh1 kwa g/100ml kwenda juu.
“Kwa mfano, ikiwa kinywaji Y kina gramu sita za sukari kwa kila mililita 100, kitavutia ushuru wa Sh2 ikiwa kimetengenezwa nchini na Sh4 ikiwa kimeagizwa kutoka nje, kwenda juu,” asema.
Anabainisha kwamba ni vinywaji vilivyo na asilimia 100 ya rojo la matunda bila kuongezewa sukari ambavyo havitatozwa ushuru.