Habari

Serikali yapanga kuongeza bei ya soda, juisi ili wananchi wadumishe afya bora

Na EDWIN MUTAI May 30th, 2025 Kusoma ni dakika: 1

BEI ya vinywaji kama soda, juisi, na maziwa ya mtindi inatarajiwa kupanda iwapo Bunge la Taifa litapitisha pendekezo la kuanzisha Ushuru wa Uimarishaji Afya.

Mbunge wa Nandi Hills, Bw Bernard Kitur, ameomba Kamati ya Bunge kuhusu Fedha kuweka ushuru huo katika Mswada wa Fedha wa mwaka 2025 kama njia ya kupunguza matumizi ya vinywaji vyenye sukari nyingi, ambavyo vinachangia ongezeko la magonjwa kama unene, kisukari na maradhi mengine yasiyo ya kuambukiza (NCDs).

“Ushuru huu unalenga kupunguza matumizi ya sukari, kuhimiza utengenezaji wa bidhaa zenye afya zaidi, na kusaidia kufadhili kampeni za afya, mipango ya lishe shuleni, na miundombinu ya afya,” alisema Bw Kitur.

Mbunge huyo alisema ushuru huo utatozwa watengenezaji na waagizaji wa vinywaji vilivyo na sukari.

Alisema viwango vyafaa kuwa gramu 4 kwa kila mililita 100 ambazo zinasamehewa ushuru ila ikiongezwa gramu yoyote kutoka hapo itavutia ushuru wa Sh1 kwa g/100ml kwenda juu.

“Kwa vinywaji vinavyoagizwa kutoka nje, viwango ni Sh2 kwa g/100ml kwenda juu,” Kitur aliambia wabunge ambao walikuwa wanapokea Maoni kuhusu mwada wa fedha.

Akaendelea kufafanua: “Ikiwa kinywaji Y kina gramu 6 za sukari kwa kila mililita 100, basi kinavutia ushuru wa Sh2 ikiwa kimetengezwa nchini na Sh4 ikiwa kimeagizwa kutoka ng’ambo.”

Alisema ushuru huo utaepukwa tu na watengezaji vinywaji vilivyo na rojo la matunda asilimia 100 bila kuongezewa sukari.