Habari

Shule kufunguliwa Jumatatu changamoto za ufadhili zikizidi

Na WINNIE ATIENO April 26th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

MAELFU ya wanafunzi wa shule za chekechea, shule za msingi, sekondari msingi (JS) na sekondari wanatarajiwa kurejea shuleni Jumatatu, Aprili 27, 2026, kuashiria kuanza kwa muhula wa pili katika kalenda ya mwaka wa masomo, huku taasisi za elimu zikikabiliwa na changamoto za kifedha.
Muhula huo, unaodumu kwa wiki 14 hadi Julai 31, ndio mrefu zaidi na wenye kazi nyingi katika kalenda ya shule. Ni kipindi muhimu ambacho walimu hutakiwa kumaliza sehemu kubwa ya silabasi, kuandaa wanafunzi kwa mitihani ya kitaifa na kutathmini maendeleo yao.
Hata hivyo, shule nyingi nchini zimebaki katika hali ngumu kutokana na ucheleweshaji na upungufu wa mgao wa serikali hali inayotishia kuathiri ufanisi wa masomo.
Wakuu wa shule wanasema wanakabiliwa na changamoto kubwa, hasa shule za kutwa zinazotegemea fedha za serikali.
“Upungufu wa fedha unakwamisha huduma muhimu, kuvuruga mipango ya masomo na kuongeza mzigo kwa wakuu wa shule,” alisema Mwenyekiti wa Chama cha Walimu Wakuu wa Shule za Sekondari Kenya( KESSHA), Willy Kuria.
Katibu wa Elimu ya Msingi, Profesa Julius Bitok, amekiri kuwepo kwa pengo kubwa la ufadhili, akisema linachangiwa na ongezeko la wanafunzi na changamoto za bajeti.
Kwa ngazi ya Sekondari Msingi, upungufu unakadiriwa kufikia Sh3.6 bilioni, huku idadi ya wanafunzi ikipanda kutoka 1 milioni hadi 2.17 milioni.
Katika sekondari, pengo la ufadhili linafikia Sh76.9 bilioni, wakati idadi ya wanafunzi imeongezeka hadi 4 milioni.
Wadau wa elimu wanasema ukosefu wa fedha za kutosha umeathiri ubora wa elimu, miundombinu na shughuli za ziada, huku wakipendekeza ruzuku maalum ya serikali kulipa madeni yaliyolimbikiza.
Wakati huohuo, utekelezaji wa mfumo wa elimu unaotegemea umilisi (CBE) umeongeza shinikizo kwa shule kutokana na mahitaji ya miundombinu na walimu zaidi.
Chama cha Walimu wa Sekondari (KUPPET) kinataka serikali kutoa mgao kamili wa fedha kwa wakati ili kuhakikisha uthabiti wa shule.
Wazazi kupitia Chama cha Kitaifa cha Wazazi wamesema wako tayari kwa muhula mpya, wakisisitiza hakuna mwanafunzi anayepaswa kukosa shule.
Serikali nayo imeonya wakuu wa shule kutowafukuza wanafunzi kwa kukosa ada au sare, ikiahidi kuchukua hatua kwa watakaokiuka agizo hilo.
Wadau wa elimu wanatahadharisha kuwa bila ufadhili wa kutosha, mfumo wa elimu unaweza kuendelea kudorora na kuathiri mamilioni ya wanafunzi nchini.