Habari

Sifuna apambana vikali na Oburu

Na JUSTUS OCHIENG' April 4th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

MVUTANO unaoendelea kati ya chama cha Orange Democratic Movement (ODM) na Katibu wake Mkuu Edwin Sifuna unaashiria dalili za kudumu kwa muda mrefu.

Bw Sifuna, ambaye ameshtakiwa kwa ukiukaji wa nidhamu ya chama, amechukua hatua ya kisheria na kisiasa kupinga uamuzi wa Baraza Kuu ya Kitaifa (NEC) ya chama kumvua wadhifa wake.

Chama kimemtaka Sifuna kujibu mashtaka ya ukiukaji wa nidhamu, ikiwa ni pamoja na kutoa kauli zinazopinga msimamo wa ODM, kushiriki katika shughuli za kisiasa bila idhini, na kutohudhuria mikutano muhimu ya chama.

Sifuna, amejipanga kwa mapambano makali huku viongozi wa chama wakimlaumu kwa ukosefu wa nidhamu.Matokeo ya mgongano huu yanaweza kubadilisha mpangilio ndani wa ODM na pia kuathiri siasa za taifa kabla ya Uchaguzi Mkuu wa 2027.

Sifuna ameitwa na chama kujibu tuhuma za ukiukaji mkubwa wa nidhamu, jambo linalohusiana na udhibiti wa chama, mwelekeo wa kisiasa, ushirikiano wa vyama, na mchakato wa urithi wa uongozi baada ya enzi ya Raila Odinga.

Katika barua iliyoandikwa Aprili 2026 na Mwenyekiti wa Kitaifa wa ODM, Gladys Wanga, Sifuna amehusishwa na mwenendo unaoonekana kuharibu umoja na nidhamu ya chama.Mashtaka yanahusisha kupinga maamuzi rasmi ya chama, kutoa taarifa zinazokinzana hadharani, kushiriki katika shughuli za kisiasa bila idhini, na kutohudhuria mikutano muhimu ya chama.

Kiini cha mgongano ni hatua Sifuna ya kukosoa makubaliano kati ya ODM na UDA, ambapo alitangaza ushirikiano kati ya vyama hivyo “umekufa.” ODM inadai kuwa matamshi hayo, yakiwemo kwenye televisheni, ni kinyume cha maamuzi ya pamoja na kudhoofisha muundo wa taasisi za chama.

Aidha, chama kinasema Sifuna alishiriki katika mpango wa “Linda Mwananchi” bila idhini—kitendo kilichoelezwa kama kuunda miundo mbadala ya kisiasa. Sifuna amepatiwa hadi Aprili 8 kutoa majibu kwa maandishi na anatakiwa kujitokeza mbele ya jopo la kinidhamu Aprili 10 2026.

Wanachama wote wa kamati ya nidhamu wamechaguliwa na Kamati Kuu ya Taifa (NEC) ambayo iliamua kuanzisha mchakato wa kumvua Sifuna na baadhi ya wachanganuzi wanasema ni sawa na mlalamishi kuwa hakimu pia.

Hata hivyo, viongozi wa chama wanasema mchakato utafanyika kwa haki.

Sifuna, ambaye mwenyewe ni mwanasheria, kupitia wakili wake, Isaac Okero, amelaani uamuzi wa NEC na ametumia Kifungu cha 88 cha Katiba ya ODM kuanzisha mgogoro rasmi.

Awali alielekeza kesi kwa Jopo la Kutatua Migogoro ya Vyama vya Kisiasa, lakini ilielekeza pande zote kutumia utaratibu wa ndani wa chama.

Mgogoro huu umechelewesha kuvuliwa wadhifa wake, na kuhakikisha anaendelea kushikilia wadhifa huo hadi utaratibu wa ndani ukamilike.Wachambuzi wa siasa wanasema mchakato wa upatanishi unampa Sifuna muda wa kuendelea kushikilia wadhifa wake.

“Hii ni fursa ya kuendeleza mjadala wa kumvua Sifuna wadhifa wake na kumfanya aonekane kama kipofu katika migogoro ya ndani ya ODM,” alisema Rachael Omollo, mchambuzi wa siasa.

Chini ya mgongano huu, ODM inaonyesha mgawanyiko mkubwa.

Kiongozi wa chama hicho Oburu Oginga amesisitiza umoja huku akionya dhidi ya ukosefu wa nidhamu.

Profesa Makau Mutua alimtaja Sifuna kama “mtu aliyekufa akitembea” ishara ya hali mbaya ya mvutano ndani ya chama hicho.

Mgogoro huu unatoa changamoto kubwa kabla ya majadiliano ya ODM na UDA kuelekea 2027.

Wachambuzi wanasema chama kilichogawanyika kinaweza kushindwa kuonyesha umoja, na hivyo kupatia UDA nafasi ya kufanikisha malengo yake.

Hata hivyo, Sifuna anaendelea kuimarisha nafasi yake kisiasa huku akikabiliwa na mchakato wa ndani wa chama.