Habari

Tuju ataka azikwe ndani ya saa 48 huku akisema hataki serikali katika mazishi yake

Na RUSHDIE OUDIA April 12th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

ALIYEKUWA waziri Raphael Tuju ameagiza familia yake imzike ndani ya saa 48 iwapo atafariki dunia, huku akipiga marufuku maafisa wa Serikali kuhudhuria mazishi yake.
Kauli hiyo ilijiri baada ya wiki kadhaa alizotaja kuwa za mateso na mfadhaiko, kuanzia kunyang’anywa mali yake mtaani Karen, kukamatwa na baadaye kulazwa hospitalini.
Tuju alisema amepitia hali ngumu ambayo imemfanya kufikiria upya uhusiano wake na Serikali ya sasa.
“Nimewaambia watu wangu wazi kwamba nikifa, nizikwe ndani ya saa 48. Sitaki kuona Serikali ikijifanya inahusika kwenye mazishi yangu. Niko tayari kwa lolote,” alisema Tuju.
Akizungumza Ijumaa katika makazi yake kijiji cha Ralingo, Ndori, Rarieda, ambapo familia iliandaa maombi maalum, Tuju alisema tayari ametambua maeneo mawili ambayo familia yake inaweza kuchagua kama mahali pa mwisho pa kupumzika iwapo atafariki.
Alisema wosia wake huo unahusu hasa utawala wa Rais William Ruto, ambao anaamini umemnyima haki.
Alikosoa namna alivyoshughulikiwa baada ya kutafuta hifadhi katika Kituo cha Polisi cha Karen, akisema alikamatwa, kudhulumiwa na baadaye kuachiliwa bila dhamana.
Tuju alisema licha ya changamoto hizo, amejiandaa kiakili kwa lolote linaloweza kumkumba.
“Nimewahi kunusurika ajali ya ndege ambapo watu walifariki, na pia nilipata ajali Limuru nikavunjika mifupa 18. Madaktari waliniambia nilikuwa na asilimia 30 tu ya kuweza kutembea tena. Lakini Mungu alinisimamia. Sio watu wanaonitisha,” alisema.
Aliongeza kuwa hana mpango wa kurejea katika siasa za uchaguzi, akisisitiza kuwa jukumu lake ni kupigania kile anachoamini kuwa haki na uwajibikaji.
“Si lazima uwe Mbunge au Seneta ili kuleta mabadiliko. Niko macho na nasikiliza wananchi, na ninaanza na kwangu Ralingo,” alisema.
Baadaye alikutana na Gavana wa Siaya James Orengo katika ofisi yake mjini Siaya, ambapo wawili hao walijadili hali ya kisiasa na masuala ya haki na utawala bora.
“Tuju amekuja nyumbani kujadiliana na mababu baada ya yale aliyopitia lakini sisi tuko pamoja naye,” alisema Orengo.
Viongozi hao pia walikosoa mipango ya kuwahamisha wakazi wa Ramula kupisha uchimbaji wa dhahabu, pamoja na mpango wa kujenga mtambo wa nyuklia Rarieda, wakitaka wananchi washirikishwe kikamilifu kabla ya maamuzi makubwa kufanyika.