Habari

Uhuru: Ruto au kiongozi yeyote hafai kujilazimisha kwa Wakenya

Na EVANS JAOLA na WINNIE ATIENO August 24th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

RAIS Mstaafu Uhuru Kenyatta na Rais William Ruto wameendeleza mvutano wao wa kisiasa huku wakitofautiana kuhusu uchaguzi wa 2027, nafasi ya upinzani na maendeleo ya serikali.
Akizungumza Jumapili katika maadhimisho ya miaka 23 ya kifo cha aliyekuwa Makamu wa Rais Michael Kijana Wamalwa, Milimani, Trans Nzoia, Bw Kenyatta alisema hana nia ya kurejea mamlakani baada ya kuhudumu kama rais kwa miaka 10.
Alisema Wakenya ndio wataamua atakayekuwa rais 2027 na hakuna kiongozi anayepaswa kuwalazimisha kumuunga mkono.
“Wakenya wataamua wanayemtaka kuwa Rais 2027. Hakuna mtu atakayewalazimisha kumuunga mkono upande wake. Tutafute kura kwa amani na uadilifu,” akasema.
Bw Kenyatta pia alitetea uhuru wa kisiasa na haki ya viongozi wa upinzani kufanya mikutano ya kisiasa, akilaani vurugu zilizotokea Homa Bay wakati wa mikutano ya viongozi wa Linda Mwananchi.
Aliwataja Kalonzo Musyoka, Fred Matiang’i, Edwin Sifuna na Rais Ruto kama baadhi ya viongozi ambao Wakenya wanaweza kuchagua kati yao katika uchaguzi ujao.
Viongozi wa upinzani waliohudhuria hafla hiyo, akiwemo Bw Musyoka, Dkt Matiang’i, Martha Karua, Charity Ngilu na Justin Muturi, walisema wako tayari kuunda muungano wenye nguvu wa kumng’oa Ruto madarakani.
Bw Musyoka alisema upinzani unafanya mipango ya kuunda muungano utakaomfanya Ruto kuwa rais wa muhula mmoja.
Kwa upande wake, Dkt Ruto aliwashutumu viongozi wa upinzani kwa kutumwa kupinga miradi yote ya serikali badala ya kutoa sera mbadala.
Alisema wapinzani wanapiga kelele kuhusu “must go”, “one term” na “Kasongo”, lakini hawana ajenda ya maendeleo.
Rais alisema serikali yake inapaswa kuhukumiwa kwa miradi na huduma inazowaletea Wakenya, badala ya misingi ya ukabila.
Akiongea katika Kaunti ya Taita Taveta, Rais Ruto alisema serikali imetenga Sh10 bilioni kushughulikia changamoto za ardhi na kuwaondoa maskwota Pwani.
 Pia alitaja ukarabati wa reli ya Voi-Taveta yenye urefu wa kilomita 129 kama mradi unaolenga kukuza biashara, utalii na ajira.
 Kule Kitale, Bw Kenyatta alimsifu marehemu Bw Wamalwa kama kiongozi mzalendo aliyependa maslahi ya taifa kuliko siasa za chuki.
Aliyekuwa waziri Musikari Kombo alisema Bw Wamalwa alikuwa kiongozi mwadilifu aliyekufa bila utajiri wa kutatanisha.
Aliyekuwa waziri Noah Wekesa alijitolea kuongoza jopo litakalosaidia upinzani kuunda muungano wa pamoja, akisema bila mgombea mmoja itakuwa vigumu kumshinda Ruto 2027.