Jamvi La Siasa

Jhanda ajitetea, adai ni haki yake ‘kuwaosha’ wafuasi wake na pesa

Na BENSON MATHEKA September 14th, 2026 Kusoma ni dakika: 1

MBUNGE wa Nyaribari Chache, Zaheer Jhanda, ametetea tabia yake ya kutoa fedha kwa wakazi wanaohudhuria mikutano yake ya kisiasa, akisema kuwa fedha hizo ni za kuwasaidia wananchi wanaosafiri umbali mrefu kufika kwenye shughuli zake za kisiasa.

Akizungumza katika mahojiano ya televisheni Alhamisi, Jhanda alisema kuwa ana uwezo wa kutoa msaada huo kutokana na mshahara wake wa ubunge pamoja na mapato anayopata kupitia biashara zake.

Kulingana naye, wananchi wengi wanahitaji maendeleo lakini pia wanahitaji fedha za kujikimu katika maisha yao ya kila siku.

Mbunge huyo alieleza kuwa si haki kwa wakazi kutoka maeneo mbalimbali kusafiri kwa gharama zao wenyewe, kuhudhuria mkutano na kisha kurejea nyumbani bila msaada wowote wa kifedha.

Alisema fedha hizo zinakusudiwa kufidia gharama za usafiri na changamoto nyingine wanazokumbana nazo wananchi wanaposhiriki mikutano hiyo.

Jhanda alihoji jinsi wazee, vijana na watu wengine kutoka sehemu za mbali wanavyoweza kuhudhuria mikutano na kurejea nyumbani bila msaada wa kifedha.

Kwa mtazamo wake, hali hiyo ni kutowatendea haki wananchi wanaojitolea kushiriki shughuli za viongozi wao.

Kauli zake zimeibua mjadala mpya kuhusu desturi ya wanasiasa kutoa fedha, chakula au bidhaa mbalimbali kwa wananchi wanaohudhuria mikutano na mikusanyiko ya kisiasa.

Wanasiasa wengi wamekuwa wakitaja misaada hiyo kama njia ya kuwawezesha wananchi au kuwashukuru kwa ushiriki wao.

Hata hivyo, baadhi ya wachambuzi wa masuala ya utawala bora na uchumi wamekosoa utamaduni huo wakisema vita dhidi ya umaskini haviwezi kushindwa kwa kugawa fedha au vifaa kwa lengo lakupata sifa za kisiasa.

Huku maandalizi ya Uchaguzi Mkuu wa 2027 yakianza kushika kasi, mjadala kuhusu nafasi ya fedha katika uhamasishaji wa kisiasa unaendelea kugawa maoni kati ya wanaounga mkono na wanaopinga mtindo huo.