Vinara wa upinzani sasa wasema Kalonzo ataweza kumenyana na Ruto
KIONGOZI wa chama cha Wiper, Kalonzo Musyoka, jana alipigwa jeki kisiasa baada ya muungano wa upinzani kupigia debe azma yake ya kuwania Urais mwaka 2027.
Vinara hao, waliofanya msururu wa mikutano katika kaunti ya Machakos, walimtaja Bw Musyoka kama kiongozi mwenye uzoefu na uwezo wa kumshinda Rais William Ruto.
Katika mikutano iliyofanyika Masinga, Matuu, Mbiuni, Kangundo, Mwala, Masii na mjini Machakos, Musyoka alionyesha kujiamini akisema yuko tayari kwa tiketi ya muungano wa upinzani kuelekea uchaguzi mkuu wa 2027, akiahidi kumpeleka Rais William Ruto nyumbani.
“Mambo yako sawa,” alisema Musyoka huku viongozi wa upinzani wakiwaomba wapiga kura wa Ukambani kumuunga mkono.
Muungano huo ulilaumu Rais Ruto kwa kile walichokiita usimamizi mbaya wa nchi na kusisitiza haja ya kumnyima muhula wa pili.
Kiongozi wa Democracy for the Citizens Party, Rigathi Gachagua, alimtaja Musyoka kama chaguo bora la kumshinda Rais Ruto, akisema ana uwezo wa kuleta ushindi.
Viongozi wengine akiwemo Eugene Wamalwa, Mbunge wa Naivasha Jayne Kihara na seneta wa zamani wa Embu Lenny Kivuti pia walimuunga mkono Musyoka. Kivuti alisema Embu yote iko nyuma ya azma yake ya urais.
Gachagua aliwataka wakazi wa Ukambani kuunga mkono Wiper kwa kuchagua wawaniaji wa chama hicho pekee kuanzia madiwani hadi rais, akidokeza uwezekano wa Musyoka kuwa mgombea urais wa pamoja wa upinzani.
Kwa upande wake, mgombea urais wa Jubilee Fred Matiang’i alisema upinzani umedhamiria kumzuia Rais Ruto kupata muhula wa pili, akimshutumu kwa kushindwa kusimamia vyema sekta za elimu, afya na usalama.
Alitaja shambulizi dhidi ya Seneta wa Vihiga Godfrey Osotsi kama ishara ya kuzorota kwa usalama nchini, akionya kuwa Kenya inaelekea katika hali mbaya ikiwa haitadhibitiwa.
Wakati huo huo, aliyekuwa Mwanasheria Mkuu Justin Muturi aliwahimiza Wakenya kujiandikisha kama wapiga kura, akisema ushindi wa upinzani unategemea ushiriki mkubwa wa wapiga kura.
Ziara ya upinzani katika maeneo ya Masinga, Matuu, Mwala, Kangundo na mji wa Machakos pia ililenga kuwahimiza wapiga kura kuwakataa wabunge wanaoegemea upande wa serikali.
Musyoka aliwaita baadhi ya viongozi wa Ukambani wanaoenda Ikulu “wasaliti” wanaopaswa kuadhibiwa kisiasa.
Hata hivyo, mkutano wa Matuu ulizua taharuki baada ya watu waliokuwa wamevalia barakoa kushambulia baadhi ya watu waliokuwa na uhusiano na Mbunge wa Yatta Robert Basil, anayedaiwa kuunga mkono serikali.
Katika eneo la Mbiuni, Musyoka pia alijibu migogoro ya ndani ya Wiper kuhusu uteuzi wa mgombea katika eneobunge la Mwala, akiahidi mchakato wa haki na wa uwazi ili kuepuka migawanyiko.
Gachagua alisisitiza kuwa Musyoka anahitaji wafuasi waaminifu ili kuepuka matatizo ya kisiasa endapo upinzani utachukua mamlaka, akitumia uzoefu wake mwenyewe kama mfano wa hatari za usaliti wa kisiasa.
Muungano wa upinzani sasa unaonekana kuongeza kasi yake nchini, ukilenga kujenga nguvu za pamoja kuelekea uchaguzi wa 2027 huku ukijipanga kuimarisha uungwaji mkono katika ngome muhimu za kisiasa.