Habari

Visingizio watumiavyo polisi kuficha mauaji vituoni sasa vyaanikwa

Na JOSEPH WANGUI June 21st, 2025 Kusoma ni dakika: 1

KUJIUA ndiko mara nyingi husingiziwa kama sababu ya kifo cha washukiwa wakiwa mikononi mwa polisi, kama ilivyotokea kwa mwalimu Albert Ojwang aliyeuawa katika kituo cha polisi cha Nairobi Central na kwa mshukiwa wa ubakaji katika Kaunti ya Kisumu.

Uchunguzi wa faili mbalimbali za mahakama zinazohusu vifo katika seli za polisi umeonyesha pia, ushirikiano wa maafisa wa polisi kuficha ukweli.

Kati ya takwimu zinazoongezeka, kesi zilizo mahakamani pia zinaonyesha kwamba, vifo vingi vinavyotokea katika seli za polisi au katika taasisi za usalama za serikali hubaki kuwa fumbo lisilotatuliwa.

Kwa mfano, katika Kaunti ya Kericho, kifo cha Jane Chepkurui katika kituo kidogo cha Polisi cha Mogogosiek katika Kaunti ndogo ya Bureti mnamo Februari 25, 2009 bado ni kitendawili baada ya Mahakama kuamua kwamba, hakuna mtu aliyeona au kusema kilichotokea.

Daktari wa uchunguzi wa maiti aliyefanya upasuaji wa maiti alieleza kuwa, uchunguzi haukuonyesha kama Chepkurui alijiua au mtu mwingine kumnyonga.

Hata hivyo, alibainisha kuwa sababu ya kifo ilikuwa ‘kukosa hewa kufuatia kunyongwa lakini haikuwezekana kuwa alijinyonga mwenyewe.”

Afisa wa uchunguzi wa kesi alisema alidaiwa kujitia kitanzi ndani ya seli za polisi kwa kutumia kitambaa ingawa hakuna mtu aliyeona mwili wake ukining’inia kutoka paa.

Pia kitambaa hicho hakikupatikana kama ushahidi. Hii ilionekana kuwa ushahidi wa uongo uliokusudiwa kuficha ukweli, mahakama ilisema.

Katika Kaunti ya Kisumu, kifo cha Samson Otieno, katika kituo cha polisi mjini mnamo Agosti 31, 2019, bado ni fumbo.

Alikamatwa kwa tuhuma za kuiba simu ya mkononi kutoka kwa mteja katika klabu cha eneo hilo.