Vita vya kandarasi vinavyonyima watoto wa Gredi 10 vitabu
MWEZI mmoja tangu wanafunzi wa Gredi 10 waripoti katika shule za Sekondari Pevu, wale walio katika shule za umma bado hawajapokea vitabu vya kiada kwa masomo yote kutoka kwa wachapishaji waliopata kandarasi ya serikali.
Kutokana na hali hiyo, walimu wamelazimika kufundisha wakitumia miundo ya mtaala iliyotayarishwa na Taasisi ya Kuendeleza Mtaala Kenya (KICD) pamoja na vitabu walivyokuwa wakitumia awali chini ya mfumo wa 8-4-4.
Kuchelewa huku kulisababishwa na mvutano kati ya wachapishaji na serikali kuhusu kutolipwa kwa madeni ya mabilioni ya pesa.
“Vitabu hivi vilikuwa tayari kuchapishwa kufikia Juni [2025] na vimekuwa vikisubiri ishara ya kuanza kusambazwa. Ishara hiyo hasa ni malipo ya madeni ya wachapishaji, ambayo pia yanahusu malipo ya wachapishaji wa mitambo na wasafirishaji,” alisema Profesa Charles Ong’ondo, Mkurugenzi Mkuu Mtendaji wa KICD, katika mahojiano mwezi Desemba 2025.
Jana, Prof Ong’ondo aliondolea lawama taasisi hiyo akisema KICD imekuwa ikizingatia ratiba katika kutathmini miswada iliyowasilishwa na wachapishaji na kutoa zabuni za usambazaji.
Uchapaishaji wa vitabu ulianza wiki ya pili ya Januari baada ya serikali kuwalipa wachapishaji Sh5.6 bilioni, ikiwa ni sehemu ya zaidi ya Sh11 bilioni za vitabu vya madarasa mengine vilivyosambazwa bila malipo kufanywa.
“Tayari tumetathmini na kuidhinisha vitabu vya Gredi 11. Tunatoa zabuni wiki ijayo Jumanne. Kwa ufadhili wa kutosha, usambazaji wa vitabu vya Gredi 11 unaweza hata kuanza Mei. Tutaanza kutathmini vitabu vya Gredi 12 mwezi Agosti mwaka huu,” alisema.
Prof Ong’ondo alisema alitarajia kupata taarifa kuhusu hali ya usambazaji jana (Ijumaa) jioni, lakini wachapishaji wamekumbwa na changamoto kadhaa mashinani.
Kushinda zabuni ya kusambaza vitabu vya kiada katika shule za umma ni biashara yenye faida kubwa kwa kuwa mchapishaji hushikilia soko la uhakika la mamilioni ya nakala kwa angalau miaka miwili. Kutokana na hilo, ushindani wa zabuni hizi umekuwa mkali sana, huku wachapishaji wakishusha bei ili kuwazidi wenzao kukiwa na madai ya ukiukaji wa taratibu.
“Kwa bahati mbaya, inaonekana baadhi ya wachapishaji waliopata zabuni hawana uwezo wa kuchapisha vitabu walivyoahidi kusambaza. Baadhi walikopa pesa ili kuchapisha na kusambaza vitabu vya Gredi 9, na serikali ilipochelewesha malipo yao, wamekuwa wakihangaika kuendelea na shughuli,” alisema mchapishaji mmoja akizungumza na Taifa Leo.