Habari

Vruuuuum! Rhino Charge yang’oa nanga Baringo

Na GEOFFREY ANENE May 30th, 2025 Kusoma ni dakika: 1

MAKALA ya 36 ya mbio za magari ya 4×4 ya Rhino Charge yaliyosubiriwa kwa hamu kubwa yatafanyika katika eneo la Saimo Soi katika eneobunge la Baringo North, Kaunti ya Baringo hapo Mei 31, 2025.

Magari 64 yameingia mashindano hayo yanayolenga kuchangisha fedha za kusaidia shirika lisilo la serikali la Rhino Ark Kenya katika shughuli zake za kuhifadhi na kulinda mazingira ikiwemo maeneo ya milima ambayo ni chemchemi ya maji.

Kwa mara ya kwanza kabisa, mashindano hayo yatashuhudia gari la kutumia umeme likitumiwa. Gari hilo kutoka timu ya EV Explorers limedhaminiwa na bidhaa ya Safaricom, M-PESA.

“Tumeshiriki mashindano haya kwa miaka 23, lakini itakuwa mara kwanza tutatumia gari la stima ambayo ni historia kwa uendelevu wa mbio za magari nchini Kenya,” akasema kiongozi wa EV Explorers, Richard Kiplagat kabla ya kuongeza kuwa mabadiliko ya tabianchi yanaathiri watu wote na pia mazingira moja kwa moja. EV Explorers pia wanadhaminiwa na benki ya KCB kwa Sh1 milioni.

Adil Khawaja wa gari nambari 44, ambaye anadhaminiwa na KCB kwa Sh10 milioni na Safaricom kwa Sh25.8 milioni, aliibuka mshindi wa kuchangisha fedha nyingi katika makala ya 35. Khawaja aliyekusanya Sh175 milioni mwaka jana, amefichua kuwa analenga tena kuibuka bora katika shughuli hiyo.

Jumla ya Sh325.8 milioni zilichangishwa mwaka jana katika eneo la Torosei, Kajiado.

Majina mengine makubwa katika makala ya 36 ni pamoja na mabingwa mara tano (Car No. 5) wakiongozwa na Graham McKittrick, washindi wa mwaka 2023 (Car No. 4) wakiongozwa na Mark Glen, Peter Kinyua (Car No. 43), Rajesh Maini (Moto Moto), Fat Rhinos, Smiling Shenzis, BATUK, Team Huzi, na Zambarau Heels on the Wheel.

Maeneo mengine ambayo yamewahi kunufaika kupitia kwa Rhino Charge ni Mlima Kenya, Aberdares na msitu wa Kakamega. Maeneo hayo yaliwekwa nyaya za stima kuzuia uharibifu.