Vyuo vikuu hatarini ardhi ya thamani ikinyakuliwa – ripoti
Ripoti ya ukaguzi imefichua uvamizi mkubwa wa ardhi katika vyuo vikuu vya umma, huku mali inayokadiriwa kuwa ya thamani ya zaidi ya Sh20 bilioni ikiwa katika hatari.
Ripoti hiyo inaonyesha kuwa vyuo vikuu vingi vya umma havina hati miliki, mikataba ya ukodishaji au stakabadhi za kuhamisha umiliki uhamisho.
Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali, Dkt Nancy Gathungu, katika ripoti yake mpya inayohusu mwaka wa kifedha unaomalizika 2024, anafichua hali mbaya.
Ripoti inasema kuwa baadhi ya ardhi imevamiwa au haijasajiliwa rasmi.
“Ukaguzi wa kumbukumbu za vyuo vikuu umeonyesha kuwa angalau vyuo vikuu vinane vya umma havina hati miliki au stakabadhi nyingine za kisheria kuthibitisha umiliki wa ardhi ya thamani ya takriban Sh20 bilioni,” inasema ripoti ya ukaguzi.
Katika Chuo Kikuu cha Egerton kilicho Njoro, ekari 2,000 zilizokuwa zimetengewa mpango wa kilimo zimenyakuliwa na mkulima asiyejulikana.
Akiongea mbele ya Kamati ya Uwekezaji ya Bunge kuhusu Utawala na Elimu mnamo Septemba 4, 2025, Makamu Mkuu wa Chuo hicho Profesa Isaac Kibwage aliomba Kamati ya Bunge iingilie kati na kusaidia chuo hicho kurudisha ardhi iliyonyakuliwa.