Wakazi Nairobi walalamikia hitilafu za usajili wa wapiga kura kuelekea Uchaguzi 2027
VINGOZI mbalimbali Kaunti ya Nairobi wameeleza wasiwasi wao kuhusu zoezi linaloendelea la usajili wa wapiga kura, wakidai kuwepo kwa kasoro zinazoweza kuathiri haki ya wananchi kushiriki uchaguzi mkuu 2027.
Wakiongozwa na Naibu Kiongozi wa Wachache katika Bunge la Kaunti ya Nairobi Bi Waithera Chege, viongozi hao wamedai kuwa baadhi ya wapiga kura wamehamishiwa na kupelekwa katika vituo vya kupigia kura vilivyo nje ya jiji la Nairobi bila ridhaa yao.
Bi Waithera alisema kuwa mbali na uhamishaji huo, pia kuna wakazi wa Nairobi wanaojisajili kwa mara ya kwanza lakini wanajikuta tayari wamesajiliwa kuwa wapiga kura katika vituo vilivyo nje ya kaunti hiyo.
Alitaja maeneo ya Embakasi Central na Embakasi West kuwa miongoni mwa yaliyoathiriwa zaidi na changamoto hiyo, huku akibainisha kuwa hali kama hiyo pia inashuhudiwa katika maeneo mengine ya jiji.
Kufuatia hali hiyo, ameitaka Tume Huru ya Uchaguzi na Mipaka (IEBC) kuchukua hatua za haraka kurekebisha dosari hizo ili kuhakikisha kila mpiga kura anasajiliwa katika kituo sahihi.
“Vijana wetu wanahitaji kushiriki uchaguzi na hawawezi kufanya hivyo kwa sababu ya hitilafu kama hizo. Hivyo, tunaomba hatua ya haraka ichukuliwe ili kutatua suala hilo,” alisema bI Chege.

Wakati huo huo, aliwahimiza wakazi kuwa makini wanapojisajili ili kuepuka hitilafu zinazoweza kuwanyima fursa ya kushiriki kikamilifu katika uchaguzi mkuu ujao.
Bi Waithera alitoa matamshi hayo alipokuwa akigawa misaada kwa wakazi wa eneobunge lake msimu huu wa Pasaka.
Katika miaka ya hivi karibuni, kumekuwepo malalamishi ya hapa na pale kuhusu hitilafu katika usajiliwa wapiga kura, ikiwemo majina ya wapiga kura kuhamishwa bila wao kujua, au kuorodheshwa katika vituo visivyo sahihi.
Changamoto hizi mara nyingi hujitokeza hasa wakati wa usajili mpya au uhakiki wa sajili.
Haya yanajiri huku IEBC ikiendeleza kampeni ya kuwarai watu wajisajili kuwa wapiga kura.
Kando na hayo, vijana wa Gen Z chini ya kaulimbiu ‘Niko Kad’i pia wamekuwa wakiendeleza kampeni kuwarai vijana nchini kujisajili kuwa wapiga kura kabla ya uchaguzi mkuu wa 2027.