Wakenya sasa hatarini kupunjwa na walaghai kupitia akaunti za simu
MNAMO 2022, kundi moja la matapeli wa mtandaoni lilitekeleza ulaghai unaodaiwa kuwa mkubwa zaidi nchini Uingereza.
Matapeli hao walitumia mtandao uliowawezesha kutumia nambari za simu za benki na taasisi za kifedha na kuwapunja takriban watu 70,000 kiasi cha hadi Sh 1.3 milioni kila mmoja.
Licha ya utapeli huo kuzimwa nchini humo mwishoni mwa 2022, utapeli sawa na huo umeibuka Kenya, matapeli wakiwekeza zaidi katika kazi yao.
Mapema wiki hii, maafisa wa upelelezi wa makosa ya jinai walinasa watu sita katika eneo la Nyali, kaunti ya Mombasa, waliodaiwa kutumia apu za kubadilisha utambulisho wa wapiga simu kufanana na zile za benki na watoaji huduma za simu nchini.
Akithibitisha kisa hicho, kamanda wa polisi kaunti Ndogo ya Nyali Moses Kirong alisema, pamoja na kitengo cha kushughulikia uhalifu wa mtandaoni, walikamata genge hilo, ambalo limewafyonza Wakenya wasio na habari fedha zao.
“Tuliwakamata watu ambao majina yao yapo kwenye ripoti ya Polisi kwa utapeli huo wa mtandaoni na tunawaomba Wakenya kuwa makini. Iwapo utapokea simu inayokupa maagizo utoe taarifa fulani muhimu kukuhusu, ni vyema ujiepushe. Kuweni waangalifu,” akasema Bw Kirong.
Mbinu yao inafanana na utapeli uliofanyika Uingereza, ambapo wanawapigia simu Wakenya na nambari zinazofanana sana na zile za kampuni husika, na kuwashawishi kutoa taarifa muhimu kama vila nambari za siri, nambari za vitambulisho na nambari ya siri ya kutumika mara moja (OTP).
Kwa mujibu wa ripoti ya polisi, kundi hilo liliwekeza zaidi ya Sh 500,000 kulipia mtandao wa kubadilisha nambari.
Pia kundi hilo lilipatikana na laini kadhaa za simu, na lilikuwa likifanyia kazi katika chumba cha kukodisha kwa muda (Airbnb).