Habari

Wakulima walilia serikali isitishe uagizaji mchele nje ili pishori ya Mwea ipate soko

Na GEORGE MUNENE May 29th, 2025 Kusoma ni dakika: 1

TAKRIBAN magunia 50,000 ya mchele wa thamani ya Sh500 milioni kutoka Mradi mkubwa wa Unyunyuzaji wa Mwea, Kaunti ya Kirinyaga, yamerundikana maghalani kutokana na ukosefu wa soko. 

Wakulima wameeleza hofu kuwa mchele wao unaweza kuoza katika maghala ya iwapo soko halitapatikana haraka.

Wakiongozwa na Mwenyekiti wa chama cha ushirika cha wakuzaji mchele Mwea Ndege Muriuki, wakulima walikiri kuwa hali ni mbaya. Walieleza kuwa walipata mavuno mengi msimu uliopita na wakaitaka  serikali kuingilia kati kuwaokoa.

“Tunateseka kwa sababu mchele wetu haujanunuliwa, hatuwezi kutimiza mahitaji yetu ya kifedha na suala hili linapaswa kushughulikiwa kwa uzito unaostahili,” alisema mkulima mmoja, Bw Charles Ngure.

Mkazi mwingine, Agnes Wagatu, alishangaa ni kwa nini serikali imeshindwa kununua mchele kutoka kwa wakulima.
“Waliahidi kununua mchele wetu lakini hakuna kilichofanyika,” alilalamika Bi Wagatu.

Bw Muriuki alitoa wito kwa serikali kuingilia kati ili wakulima wasipate hasara kubwa. Alilaumu ukosefu wa soko kwa bidhaa za hapa nchini kwa uagizaji wa mchele wa bei nafuu kutoka nje ya nchi.

“Serikali imekubali kuingizwa kwa mchele wa bei ya chini, hali inayofanya iwe vigumu kwa mchele wetu wa pishori kupata soko. Uagizaji huu unapaswa kudhibitiwa ili tupate soko kwa bidhaa yetu ambayo tumetumia fedha nyingi kuizalisha. Hili limeleta mgogoro mkubwa katika mradi huu mkubwa,” alisema Bw Muriuki.

“Wakulima hawawezi kulipwa kwa sababu chama hakijauza mchele wao. Hawa ndio wakulima wanaozalisha zaidi ya asilimia 80 ya mchele unaoliwa Kenya na wanapaswa kusaidiwa. Wanategemea mchele huo kuwalisha na kuwasomesha watoto wao pamoja na kutimiza mahitaji mengine ya kifedha. Kwa sasa, wanateseka,” aliongeza.

Wakulima pia walilalamika kuwa mabroka wameanza kurejea katika mpango huo baada ya kugundua kuwa hakuna soko la mchele.

“Mabroka tayari wamewasili na wanataka kununua mchele wetu kwa bei ya chini sana. Wanajua kuwa tuko kwenye hali ngumu na wanataka kutumia nafasi hii kutufyonza,” alisema mkulima mwingine.