Yafichuliwa jinsi maafisa wa elimu wanavyokausha shule
MAJADILIANO katika Bunge la Kitaifa alasiri ya Jumatano kuhusu mgao wa pesa shuleni kutoka kwa serikali yalifichua jinsi maafisa wa elimu wanavyoendelea kufyonza fedha za shule za umma.
Hii inawaacha wakuu wa shule bila chaguo ila kuendelea kuwatuma wanafunzi nyumbani wakiwataka walete pesa kwa shughuli mbalimbali ambazo tayari zimefadhiliwa na serikali.
Kulingana na wabunge, msururu huu wa “utapeli” huanza mara tu maafisa wanapogundua kuwa pesa za serikali tayari zimeingia katika akaunti za shule.
Kuanzia wakaguzi wa shule, wakaguzi wa hesabu, hadi makundi mbalimbali yanayodai kuandaa shughuli za shule, barua huanza kumiminika katika shule hizo zikitaka fedha kwa sababu mbalimbali.
Mjadala huu ulianzishwa na jibu kutoka kwa Kamati ya Elimu ya Bunge la Kitaifa kuhusu swali lililoulizwa na Naibu Kiranja wa Wachache Robert Mbui kuhusu mgao kwa shule.
Mpango wa kufuja fedha za umma pia unawahusisha wakuu wa shule, ambao hufungua akaunti za benki nje ya akaunti rasmi za shule, wakidai kuwa wanaandaa shughuli za michezo. Akaunti hizi hazikaguliwi kwa kuwa hazitambuliwi rasmi, jambo linalofanya matumizi ya fedha hizo kuwa ya kutiliwa shaka.
“Wanaendesha akaunti kama za ‘Shughuli za Michezo ya Wakuu wa Shule wa Kilifi’ – pesa zinazowekwa na walimu wakuu huko hazikaguliwi,” alisema Mbunge wa Kilifi Kaskazini Owen Baya.
“Nataka Kamati ya Hesabu za Umma ichunguze shule. Katika eneo bunge langu, kuna tatizo hili. Pesa zikipelekwa shule, barua huja kutoka kwa ofisi ya elimu ya kaunti ndogo ikidai kiasi fulani kwa kila mwanafunzi — iwe ni Sh10 au Sh5 — kwa shughuli mbalimbali,” aliongeza Baya.
Kwa mfano, serikali hutenga Sh140 kwa kila mwanafunzi wa Sekondari ya Msingi kwa shughuli za ziada. Hata hivyo, shule huishia kubaki na Sh25 pekee kwa kila mwanafunzi baada ya kutoa Sh85 kwa ofisi ya kaunti ndogo kwa uratibu, Sh20 kwa ofisi ya elimu ya kaunti ndogo, na Sh10 kwa chama cha eneo.
Shughuli za shule hufadhiliwa katika viwango vitano: kitaifa, mkoa, kaunti ndogo, na eneo la shule.
“Kuna watu wanaojitajirisha sana kutokana na pesa za shule. Hali hii lazima ikomeshwe. Fedha zinazotolewa na serikali lazima ziwanufaishe watoto wetu, si watu binafsi,” Baya alisema.
Aliongeza kuwa amepokea malalamiko kutoka kwa walimu wakuu katika eneo bunge lake waliotaka wasitajwe kwa kuhofia kisasi kutoka kwa maafisa wa elimu wa kaunti na kaunti ndogo.
“Walimu wakuu wanateseka. Ukikataa kutii maagizo yaliyoandikwa kwenye barua, unaadhibiwa,” alisema Baya.
Taifa Jumapili liliona akaunti tatu za aina hii katika Kaunti ya Kilifi zilizofunguliwa katika moja ya benki kubwa. Kuna akaunti ya uratibu wa shughuli za ziada kwa shule za msingi za kaunti na ya tathmini.
Wabunge walihoji kwa nini shule zinatakiwa kupeleka pesa kwa kila mwanafunzi kwenye vyama hivi ilhali serikali tayari hutoa fedha za kugharamia shughuli hizo.
Baadhi ya maafisa wamelaumiwa mara kwa mara kwa kudai hongo kutoka kwa shule huku walimu wakuu wakiripotiwa kulipa hadi Sh50,000 kwa kila ziara kulingana na kiwango cha shule ili kupata ripoti nzuri za ukaguzi.
Ukaguzi wa shule pia umetajwa kama chanzo cha uporaji. Ingawa unafadhiliwa na wizara, wakaguzi hudaiwa kupokea takriban Sh40,000 kutoka shule kwa mahitaji yao ya malazi, fedha ambazo hutolewa kutoka mgao wa serikali.
Wabunge pia walidai kuwa sehemu ya pesa za mgao hutumika kufadhili shughuli za Chama cha Wakuu wa Shule za Sekondari Kenya (KESSHA).
“Isipokuwa Bunge lichukue hatua kali na kuagiza ukaguzi maalum wa fedha za shule na ofisi za elimu za kaunti, wanafunzi wetu wataendelea kuteseka na kutumwa nyumbani kwa sababu zisizo na msingi,” alionya Baya.
“Kile ambacho wizara husema hapa Nairobi si kile kinachotokea mashinani. Bunge lazima lichukue hatua kuchunguza shule,” aliongeza.
Mbunge wa Imenti ya Kati Moses Kirima alisema walimu wamezoea kuwatuma wanafunzi nyumbani kwa sababu ya ada ambazo hazikubaliwi na Sheria ya Elimu ya Msingi.