Habari Mseto

Kesi ya jaji aliyetupa kesi iliyomkabili Pattni kusikizwa upya na Mahakama ya Juu

May 17th, 2018 1 min read

Na RICHARD MUNGUTI

MAHAKAMA ya Juu Jumatano iliahirisha kusikizwa kwa kesi ya Jaji Joseph Mbalu Mutava aliyefutwa kazi kwa kutupilia mbali kesi dhidi ya bwanyenye Kamlesh Pattni ya wizi wa Sh5.8 bilioni kutoka kwa Serikali miaka 26 iliyopita.

Wakiongozwa na Jaji Mkuu David Maraga majaji wa Mahakama ya Juu waliamuru kesi hiyo isikizwe Julai 18, 2018.

Jaji Mutava aliwasilisha kesi kupinga kutimuliwa kazini na jopo iliyoteuliwa na Rais Uhuru Kenyatta.

Kesi hiyo iliahirishwa baada ya korti kufahamishwa na wakili Kyalo Mbobu kwamba wakili Philip Nyachoti anayemwakilisha Jaji Mutava anawakilisha Magavana katika kesi za uchaguzi.

Bw Nyachoti alikuwa anaendeleza kesi hizo katika Mahakama  ya Rufaa, Eldoret.

Wakili huyo anasema jopo la majaji iliyoongozwa na Jaji Maraga kabla ya kuteuliwa kuwa Jaji Mkuu ilikosea kumpendekezea Rais Kenyatta amfute kazi Jaji Mutava.