Dimba

Kichuna atumia chale kumshawishi Bellingham ampe ‘mechi’

Na CHRIS ADUNGO July 13th, 2024 2 min read

KATIKA juhudi za kumtia Jude Bellingham kishawishini, mwanamitindo mmoja raia wa Brazil amechanja chale ya kudumu yenye jina na mchoro wa sura ya nyota huyo wa Uingereza karibu na sehemu zake za siri.

Kipusa Tyffany Santos alisema shabiki wake mmoja aligharimia shughuli hiyo kwa Sh1.2 milioni kabla ya mechi ya nusu-fainali ya Euro 2024 iliyoshuhudia Uingereza wakipepeta Uholanzi 2-1 mnamo Jumatano usiku. Ushindi huo ulikatia Uingereza tiketi ya kuvaana na Uhispania kwenye fainali ya kesho jijini Berlin, Ujerumani.

Tyffany anajulikana pia kwa kuuza picha na video za uchi wake kwenye jukwaa la mtandaoni la OnlyFans. Alivalia jezi ya Uingereza alipokuwa akichanjwa chale hiyo ambayo sasa huenda ikasambaratisha uhusiano wa kimapenzi kati ya Bellingham na kisura wake raia wa Uholanzi, Laura Celia Valk.

Kwa mujibu wa Tyffany, hatua yake ya kuchora jina na sura ya Bellingham chini ya kitovu ni kumchochea kiungo huyo wa Real Madrid kufanya hima na adokoe tunda ambalo amemhifadhia kwa muda mrefu.

“Sikuwahi kufikiria kuwa ningepata fursa hii ya kumtumia Bellingham ombi maalumu la kumtaka aonje asali ya mzinga huu ambao nimemwekea kwa kipindi kirefu. Natamani kumburudisha chumbani, anivishe pete ya ndoa na niishi naye raha mustarehe,” akasema Tyffany.

Alipoulizwa na mashabiki wake kwenye Instagram iwapo hajui kwamba Bellingham anatoka sasa kimapenzi na Laura, kisura huyo alijibu:

“Ninapenda kufanya vitu tofauti na vya kushangaza watu. Ninachohitaji ni dakika mbili tu na Bellingham na atamsahau kabisa huyo mrembo wake milele.”

Mwezi jana, Tyffany aliahidi kuwapa wanasoka na mashabiki wa timu ya taifa ya Brazil “burudani ya kipekee” iwapo kikosi hicho kingefaulu kutwaa taji la Copa America mwaka huu.

Tyffany alitoa ahadi ya kuvua nguo na kusalia uchi wa mnyama ili kusherehekea ufanisi huo wa Brazil ambao kinyume na matarajio walidenguliwa na Uruguay kwa penalti 4-2 kwenye robo-fainali baada ya sare tasa Jumapili iliyopita.

Wakati huo, Tyffany aliahidi kutia mchoro wa kudumu wa jina ‘NeyVini’ (ufupisho wa Neymar na Vinicius Jr) kwenye makalio kisha kuchanja chale zenye sura za wanasoka hao wawili kifuani pake iwapo wawili hao wangeshindia Brazil taji la Copa America mwaka huu.

Tyffany baadaye alirekodi video akiwa uchi katika uwanja wa Underground jijini London huku cha pekee kilichomsitiri zikiwa ni rangi za bendera ya Brazil alizokuwa amepakwa mwilini.

“Alijifunika mwili kwa rangi zilizojichora kwa mtindo wa sare ya timu. Alitumia muda wa zaidi ya saa nne kuchora mwili wake hadi akapata mwonekano huo,” kituo cha Odia nchini Brazil kilifichua.