Kitovu cha Lugha

Ni upi mustakabali wa lugha za Kiafrika katika teknolojia na enzi ya leo ya Akili-Unde?

April 9th, 2026 Kusoma ni dakika: 1

AFRIKA ina zaidi ya lugha 2,000 ambazo ni thuluthi moja ya lugha zote ulimwenguni. Miongoni mwa lugha hizi ni Kiswahili – lingua franca ya Afrika Mashariki, Kiyoruba, Amharic, isiZulu na Kisomali.

Lugha hizi na nyingine nyingi zinasimba (encode) kanzi kubwa ya maarifa ya kiasili, masimulizi mbali na kuwa vitambulisho vya tamaduni za jamii mbalimbali.

Hata hivyo, wataalamu wa lugha wamebaini kwamba setidata Kuu za programu zinazohusu Uchakataji wa Lugha Asilia – Natural Language Processing (NLP) kama vile Common Crawl, Wikipedia na OpenSubtitles hupendelea pakubwa lugha za Ulaya.

Kwa mfano, Kiingereza pekee kinaweza kuchangia zaidi ya asilimia 50 ya matini kwenye programu hizo, huku takriban lugha zote za Kiafrika zikichangia chini ya asilimia 0.1.

Hata lugha za Kiafrika kama Kiswahili hazina data ya kutosha katika mianda hiyo.

Mtaalamu Rocha Chimerah, katika kitabu chake – Kiswahili: Past, Present and Future Horizons (NUP, 2000) anasema: “Imetabiriwa kwamba, katika karne ya 21, lugha ambazo hazitakuwa na msamiati wake kwenye kompyuta zitaachwa nyuma na hatimaye kufa.”

Kwa bahati nzuri chambilecho Chimerah, Kiswahili hakimo katika mkumbo wa lugha hizo.

Huku suala la Akili Unde (AI) likiendelea kushika kasi katika ubainishaji wa mabadiliko ya kidijitali, wataalamu wa lugha za Kiafrika wanapaswa kutafakari upya kuhusu mustakabali wa lugha hizo katika mwanda huu.

Inatia moyo kwamba Kenya, Afrika Kusini, Naijeria na Ghana zimepiga hatua katika kujaribu kukita nanga ya Akili Unde kwenye mikakati yao ya maendeleo.

MAKALA YATAENDELEA…