Habari

Maafisa wa EACC wafanya msako nyumbani kwa Gavana Waititu

May 23rd, 2019 1 min read

Na MWANDISHI WETU

MAAFISA wa Tume ya Maadili na Kupambana dhidi ya Ufisadi (EACC) wamefanya msako Alhamisi katika nyumba ya Gavana wa Kiambu, Ferdinand Waititu, iliyoko mtaani Kileleshwa, Nairobi.

Maafisa hao waliofika kwa makumi, waliingia katika makazi hayo ya Bellcrest Gardens, kando mwa barabara ya Githunguri, dakika chache tu baada ya saa kumi na moja alfajiri na kuanza kupekua wakitafuta faili na stakabadhi.

Upelelezi wa EACC ulidai kuwepo kwa ufisadi katika kaunti yake ambayo inapakana na ile ya Nairobi ambalo ni jiji kuu la Kenya.

Aidha, walikuwa wanatafuta stakabadhi muhimu zinazohusiana na kandarasi ambazo zilitolewa na utawala wa Bw Waititu.

Gavana huyo amemulikwa na EACC kuhusiana na madai ya ufisadi kugubika mipango kadha ya serikali ya kaunti ikiwa ni pamoja na ule wa Kaa Sober ulionuia urekebishaji mienendo na kuzima uraibu wa pombe miongoni mwa waathirika.

Vyanzo kadhaa vimeambia Taifa Leo kwamba maafisa wengine 15 wa serikali ya kaunti hiyo wamemulikwa katika uchunguzi unaoendelea.

Tutakuletea habari kwa kina.