• Nairobi
  • Last Updated May 13th, 2024 7:02 PM
AFYA: Cha kufanya ili kuzuia fangasi miguuni

AFYA: Cha kufanya ili kuzuia fangasi miguuni

Na MARGARET MAINA

[email protected]

WATU wengi wanaoishi katika maeneo yenye joto la wastani mpaka la juu ni kundi la watu wanaokabiliwa na maambukizi ya fangasi katika ngozi ya miguuni.

Mara nyingi ngozi ya miguuni hasa ya nyayo na katikati ya vidole huanza kuwa na vimelea na fangasi.

Uwepo wa unyevunyevu na joto huwa ni chanzo kubwa cha kuwepo kwa fangasi miguuni.

Watu ambao wako katika hatari ya kupata fangasi miguuni ni wale wenye kiasi kikubwa cha tezi zinazotoa jasho nyayoni.

Wengine ni wenye kinga dhaifu, wanaugua kisukari, wanaoishi maeneo yenye joto kali na wale wanaovaa viatu kwa muda mrefu.

Maambukizi haya yanaweza kuwa chanzo cha kupata fangasi maeneo mengine ikiwamo katika sehemu za siri, viganja vya mikono na mwili mzima.

Uwapo wa fangasi miguuni unaweza pia kumhatarisha mwathirika kuvamiwa na bakteria kwenye ngozi ambao wanaingia ndani ya ngozi na kuleta madhara.

Fangasi husambaa na kuambukizwa kutoka kwa mtu mmoja hadi mwingine kwa kugusana na vitu vilivyotumiwa na mwenye vimelea aina ya fangasi.

Katika maisha ya kila siku mara nyingine watu huvalia soksi na kisha viatu. Hii ni mojawapo ya njia zinazoweza kueneza maambukizi ya fangasi wa miguuni kwa wanaoishi mazingira ya pamoja.

Si hivyo tu bali pia kuvaa viatu na soksi za mitumba ambavyo kwa pamoja pengine vimetumiwa na mtu aliyekuwa na fangasi.

Vilevile kukanyanga sakafu au vitu vilivyokanyagwa ikiwamo mazulia, mabwawa ya kuogelea, vifaa vya mazoezi vilivyotumiwa na mtu aliye na fangasi hiyo huhatarisha mtu.

Dalili

Dalili kubwa ya fangasi ni muwasho unaokulazimisha kujikuna, harufu mbaya ya muozo katika miguu, na kumomonyoka ama kulika kwa ngozi yenye fangasi.

Pia kuvuja kwa majimaji yenye kuteleza na harufu nzito, maumivu au kuhisi kuchomachoma baada ya kuchubuka na pia mara nyingine kuhisi joto kwenye eneo lililovamiwa na fangasi.

Ugunduzi wa fangasi wa ngozi ya miguu ni rahisi, huhitajiki kwenda maabara kwa sababu wahudumu wa afya wanaweza kugundua kwa kupata historia ya dalili na kutazama kwa macho.

Mara nyingine unaweza usihitaji kupewa dawa za kukabiliana na fangasi wa miguu, elimu ya afya inaweza kukubadili tabia na ukadhibiti fangasi wa ngozi ya miguuni bila dawa.

Njia za kukabili fangasi

Mojawapo ya njia rahisi za kukabiliana na kujikinga na fangasi ni kubadili mienendo ya kimaisha ikiwamo kupenda kuwa nadhifu hasa kimwili pamoja na kufua nguo zinazovaliwa ikiwamo soksi ambazo wengine huzivaa kwa muda mrefu bila kuzifua.

Matibabu ya dawa za fangasi za kupaka zilizo katika mtindo wa poda pia ni muhimu.

Hakikisha pia ukiwa una tatizo hili kiasi cha kufikia kupata vidonda miguuni, unapata chanjo ya tetenasi.

You can share this post!

AIBU YA UBAGUZI: Moussa Marega wa FC Porto ajiondoa uwanjani

AFYA: Faida za majani ya giligilani/ korianda katika mwili...

adminleo