• Nairobi
  • Last Updated May 3rd, 2024 4:40 PM
AFYA: Hatua za kumsaidia mjamzito kupunguza kichefuchefu

AFYA: Hatua za kumsaidia mjamzito kupunguza kichefuchefu

Na MARGARET MAINA

[email protected]

MIEZI mitatu ya kwanza ya ujauzito, ni muda wa mabadiliko mbalimbali kimwili na kisaikolojia kutotokana na homoni za uzazi kuzalishwa kwa wingi zaidi.

Mabadiliko haya hutofautiana kutoka kwa mwanamke mmoja hadi mwingine, na pia kwa mwanamke mmoja kwa nyakati tofauti.

Kipindi hiki cha ujauzito, mwili wa mama unatengeneza homoni kwa wingi.

Ni vigumu sana kuzuia hii hali kwa mjamzito kwa sababu ni mabadiliko ya mwili ya kuuandaa kuweza kupokea kiumbe kijacho.

Ingawa hivyo, unaweza kupunguza kiasi tatizo na madhara yake.

Kula kidogo mara nyingi zaidi kwa siku

Ni vizuri kula kidogo kidogo mara nyingi kuliko kula chakula kingi kwa milo mitatu kwa siku. Kula mara nyingi husaidia kuongeza sukari mwilini sababu hali ya uchovu na ugonjwa huweza kusababishwa na kutokuwa na sukari ya kutosha kwenye damu. Sukari ndio chanzo cha nguvu mwilini. Chakula cha mara kwa mara humpa mama kiasi cha nguvu za kutosha kwake na kwa mtoto kwa muda wote.

Andaa chipsi za viazi

Chumvi iliyomo kwenye viazi husaidia kukausha mate ambayo huwafanya baadhi ya wajawazito kuhisi kutapika mara kwa mara. Pia, wanga katika viazi husaidia kurekebisha kiwango cha sukari kwenye damu.

Tumia limau au ndimu

Limau au ndimu vina uchachu ambao husaidia kukata hali ya kichefuchefu. Kata limau na unuse harufu ya tunda hili. Kufanya hivyo kutasaidia kupunguza hii hali ya kutapika. Pia unaweza ukakamulia limau kwenye chai au maji ukanywa. Unaweza pia kunusa maganda au majani ya limau maana husaidia pia kupunguza hali ya kichefuchefu.

Kula vyakula venye protini na vitamini B6

Vyakula venye protini kwa wingi na vile vyenye vitamini B6 humfanya mama apunguze hali ya kichefuchefu. Inashauriwa mjamzito aepuke kula vyakula venye viungo vingi, mafuta au vilivyokaangwa kwa muda mrefu sana. Vyakula hivi vinaweza kuzidisha hali ya kichefuchefu na mtu kuhisi kutapika.

Tangawizi

Tangawizi hupunguza hali ya kichefuchefu na hivyo unaweza kuitumia kwenye chai. Kuwa makini na hakikisha unatumia tangawizi kiasi na wala sio nyingi.

Kula kifungua kinywa kabla ya kutoka kitandani

Mjamzito anashauriwa apate kifungua kinywa akiwa bado kitandani. Hali ya kuamka na tumboni hakuna kitu huweza kuwa chanzo cha kuhisi kichefuchefu na kutapika.

Kunywa maji mengi

Kunywa maji mara kwa mara ili kuzuia mwili kuishiwa na maji (dehydradtion). Ni vizuri kunywa lita 2.5 kwa siku ikiwa pamoja na maji, chai au juisi za matunda zisizo na sukari ya kuongezewa au kemikali za viwandani.

Kunywa pregnancy multivitamin

Wakati mwingine ni vizuri kumwona daktari ili kupata maelekezo ya dawa ambazo ni salama kuzitumia kupunguza hali ya kutapika. Pia kama kuna uwezekano wa kupata dawa zinazoweza kurudisha virutubisho muhimu mwilini, ikiwa ni pamoja na folic acid na vitamini D, basi tumia. Tahadhari usitumie dawa bila ushauri wa daktari.

You can share this post!

SIHA NA LISHE: Pilipili zina faida lakini pia madhara yapo

AFYA: Madhara ya uvutaji sigara

adminleo