Afya na Jamii

Maambukizi ya ukambi yaongezeka duniani chanjo ya kinga ikipungua

Na BENSON MATHEKA, THE CONVERSATION June 13th, 2025 Kusoma ni dakika: 2

WATU wanaougua ukambi wamekuwa wakiongezeka duniani katika miaka ya hivi karibuni. Mnamo mwaka wa 2023, kulikuwa na visa milioni 10.3 duniani kote ongezeko la asilimia 20 ikilinganishwa na mwaka wa 2022.

Mlipuko wa ukambi au surua, umeshuhudiwa katika maeneo mengi duniani ikiwemo Amerika, Ulaya na Australia. Kwa mfano, ripoti zinaonyesha kuwa Vietnam imekuwa na maelfu ya kesi za surua katika miaka ya 2024 na 2025.

Nchini Australia, visa 77 vya ugonjwa huu vilirekodiwa katika miezi mitano ya kwanza ya mwaka 2025, ikilinganishwa na visa 57 mwaka mzima wa 2024. Visa vingi vya ukambi nchini Australia zinahusiana na usafiri wa kimataifa,hutokea kwa wasafiri wanaorejea kutoka nje au kuambukizwa ndani ya nchi baada ya kukutana na msafiri aliyeambukizwa au watu waliokutana naye.

Ukambi huathiri sana watoto na inaweza kuzuiliwa kwa chanjo. Nchini Australia, chanjo ya surua hutolewa kwa dozi mbili – ya kwanza akiwa na miezi 12, na ya pili akiwa na miezi 18. Lakini kutokana na mlipuko mkubwa duniani, je, kuna haja ya kuangalia upya utoaji wa chanjo hii?

Ukambi husababishwa na virusi vya aina ya Morbillivirus. Dalili zake ni pamoja na homa, kikohozi, mafua na upele. Ingawa mara nyingi huonekana kama ugonjwa wa kawaida, surua inaweza kusababisha hali mbaya inayohitaji kulazwa hospitalini au hata kusababisha kifo. Mlipuko mkubwa unaweza kulemaza mfumo wa afya.

Ugonjwa huu unaweza pia kusababisha madhara makubwa ya kiafya, ikiwemo kwenye ubongo na mfumo wa kinga, hata miaka kadhaa baada ya kuambukizwa.

Ugonjwa huu huenea kwa urahisi kupitia matone madogo ya hewa yanayotoka kwa mtu aliyeambukizwa. Matone haya yanaweza kubaki angani kwa hadi saa mbili. Mtu mmoja aliyeambukizwa anaweza kuambukiza watu 12–18 wasio na kinga.

Kwa sababu ya uwezo wake mkubwa wa kuambukiza, Shirika la Afya Duniani (WHO) linapendekeza kuwa angalau asilimia 95 ya watu wachanjwe dozi mbili ili kuzuia kuenea kwa ugonjwa huu na kufikia kinga ya jamii.

Chanjo duni au kushuka kwa viwango vya chanjo – hasa baada ya janga la Covid-19 – ndicho chanzo kikuu cha milipuko ya sasa ya Ukambi kote duniani.

WHO inapendekeza kila mtu apate dozi mbili za chanjo ya ukambi. Katika maeneo yenye maambukizi mengi, watoto wanashauriwa kupewa dozi ya kwanza wakiwa na miezi tisa, kwa kuwa hadi kufikia umri huo kinga ya mama huwa imepungua kwa kiwango kikubwa na mtoto huwa hatarini kuambukizwa.