Makala

Ajabu kaunti ikilipa Sh10.7 bilioni kama ada kwa mawakili

Na NDUBI MOTURI Na KEVIN CHERUIYOT June 20th, 2025 Kusoma ni dakika: 2

MADIWANI wa kaunti ya Nairobi wanachunguza visa ambapo serikali ya kaunti hiyo ililipa mawakili Sh10.7 bilioni kama ada za huduma za kisheria, kwa njia ya kutatanisha.

Kwanza, serikali ya kaunti ya Nairobi ilitozwa Sh34 milioni na kampuni ya mawakili ya Momanyi and Associates iliyoiwakilisha katika kesi ambapo ilishtakiwa na kampuni ya Yellow Horse Inn Ltd iliyodai kuwa serikali hiyo iliipokonya ardhi yake.

Kampuni hiyo ilidai kuwa serikali ya kaunti iliidai ada ya ardhi ya kima cha Sh5.3 milioni lakini baadaye serikali hiyo ilidai ardhi hiyo ni mali yake.

Mali hiyo iliyoko katikati mwa jiji iliorodheshwa kama ya kibinafsi katika rekodi za kaunti ya Nairobi.

Lakini baadaye kampuni ya  Yellow Horse Inn Ltd, iliishtaki kaunti hiyo kwa kuorodhesha mali yake visivyo.

Kesi ilipokuwa ikiendelea, serikali ya kaunti ya Nairobi ilibadili msimamo na kudai ndio mmiliki halisi wa kipande hicho hicho cha ardhi.

Ni katika kesi hiyo ambapo serikali ya kaunti ya Nairobi iliwakilishwa na kampuni ya mawakili ya Momanyi and Associates ambayo awali iliitisha Sh80 milioni lakini baadaye ikapunguza kiasi hicho hadi Sh34 milioni.

Hata hivyo, hamna stakabadhi hitajika, kisheria, zilizowasilishwa kuhalalisha gharama hiyo. Stakabadhi hizo ni; kandarasi, risiti ya kudai malipo (invoice), taarifa ya kisheria au barua rasmi.

Sasa madiwani wa Nairobi wanadai kuwa mzozo kati ya serikali ya kaunti na kampuni ya Yellow Horse Inn Ltd, ulikuwa wa kubuniwa na hivyo ni njama ya kampuni za mawakili na maafisa wa kaunti kufyonza pesa za umma.

Katika kesi nyingine, Serikali ya Kaunti ya Nairobi ilishtakiwa kwa madai kuwa iliruhusu maovu kama vile utoaji hongo wakati wa usajili wa maafisa wa kuongoza magari katikati mwa jiji.

Kampuni ya mawakili ya Gitunda Mariti and Company Advocates ilikodiwa kuitetea serikali ya kaunti ya Nairobi.

Kampuni hiyo ilitoza ada ya Sh100 milioni, kiasi ambacho baadaye kilipunguzwa hadi Sh67 milioni, pesa ambazo zililipwa Juni 20, 2023.

Isitoshe, Sh30 milioni zingine zililipwa kwa kampuni nyingine ya mawakili, bila kuwepo kwa stakabadhi hitajika kisheria kama vile kandarasi.

Madiwani wa Nairobi sasa wanachunguza malipo hayo kwa mawakili, wakidai ni njia haramu za kufyonza pesa za umma kupitia utozaji ada za juu kupita kiasi.

Wakati huu, jumla ya kampuni 11 za mawakili zinadai Sh10.7 bilioni kutoka kwa serikali ya kaunti ya Nairobi kwa kutoa huduma za kisheria.

Uchunguzi huo unaendeshwa na Kamati ya Bunge  la Kaunti kuhusu Uhasibu (CAPAC) inayoongozwa na Diwani wa Ngara Mwaura Chege.

“Ikiwa serikali kaunti inaweza kuitisha ada za ardhi kutoka kwa mtu fulani kisha baadaye inadai kuwa ndio mmiliki halisi wa ardhi hiyo, sio hii inaashiria kuwa ilifeli kufanya uchunguzi wa mapema inavyohitajika kisheria?”, akauliza.

Kwa upande wake Diwani wa Baba Dogo Geoffrey Majiwa aliishutumu serikali ya kaunti ya Nairobi kwa kile alichotaja kama hatua yake ya “kujiingiza katika kesi nyingi zisizo na maana.”

“Kipande hicho cha ardhi katika eneo la Ruaraka kilitengewa ujenzi wa kituo cha zima moto. Lakini, serikali ya kaunti bado ilidai ada ya ardhi ambayo ililipwa. Baadaye ardhi hiyo iliuzwa. Sasa kituo cha kibinafsi cha zima moto kimejengwa katika ardhi ya umma na serikali ya kaunti imeelekea kortini kudai umiliki wa ardhi hiyo hiyo,” akasema Bw Majiwa.