Nchi wanachama wa Comesa zatakiwa kusanifisha sera za mbegu kukabili njaa
NCHI wanachama wa Soko la Pamoja la Afrika Mashariki na Kusini (COMESA) zimetakiwa kusanifisha sera na kanuni za mbegu ili kukabiliana na kero ya uhaba wa chakula.
Takwimu za COMESA zinaonyesha kuwa ni asilimia 20 pekee ya wakulima wa mashamba madogo – milioni 90 walioko katika ukanda huo wanaopata mbegu bora na zilizoboreshwa.
Hii imewaacha watu milioni 130 kati ya jumla ya watu milioni 610 wanaoishi nchi 21 zinazounda muungano wa COMESA wakiishi katika umaskini na kukumbwa na uhaba wa chakula.
Tatizo kuu ni soko la mbegu lililogawanyika, ambapo kila nchi inatumia sera na sheria zake. Hali hii inasababisha changamoto kwa kampuni za mbegu kupanua biashara zao katika nchi jirani.

“Kampuni za mbegu hulazimika kuingia katika kila soko la kitaifa kivyake, jambo ambalo ni ghali na linalosababisha ucheleweshaji wa usambazaji mbegu bora kwa wakulima wadogo,” anasema Dkt John Mukuka, Mkurugenzi Mkuu wa ACTESA, shirika maalum la COMESA.
Dkt Mukuka anabainisha kuwa, licha ya uwepo wa soko la mbegu lenye uwezo wa tani milioni 2, nchi za COMESA huzalisha na kupata chini ya tani 500,000 pekee—sawa na asilimia 2 ya uzalishaji wa kimataifa wa mbegu.
Akizungumza katika mkutano wa kikanda wa utekelezaji wa Mpango wa Usanifishaji wa Mbegu wa COMESA, ndio Seed Harmonisation Implementation Plan (COMSHIP) uliofanyika jijini Nairobi majuzi, Dkt Mukuka alisisitiza umuhimu wa kusanifisha sera na kanuni ili kuziba pengo lililopo.
Kupitia ACTESA, COMESA imeanzisha kanuni za pamoja za biashara ya mbegu.

Mpango wa COMSHIP, Regional Enterprise Competitiveness and Access to Markets Programme (RECAMP) – unaofadhiliwa kupitia 11th European Development Fund (EDF), unatekelezwa kusaidia uharakishaji wa utekelezaji wa kanuni hizo katika ngazi ya kitaifa na kikanda.
Lengo kuu la COMSHIP ni kuongeza uzalishaji wa mbegu, kuhakikisha ubora, na kuimarisha biashara ya mbegu katika ukanda wa Afrika Mashariki na Kusini.
Pia, shabaha yake ni kuongeza ushindani katika sekta ya mbegu Afrika Mashariki na Kusini. Wakati wa mkutano huo, wadau walikubaliana kuanza kutumia lebo ya mbegu ya COMESA kwa ajili ya utambuzi wa kitaifa na kikanda.
Dkt Mukuka alitaja mafanikio yaliyopatikana tangu mwaka 2015, ikiwa ni pamoja na usajili wa aina 119 za mbegu kutoka kampuni 20 na taasisi za utafiti kama vile CGIAR.

CGIAR ni muungano unaoleta pamoja mashirika ya kimataifa yanayohusika kwenye ajenda ya kuangazia usalama wa chakula duniani.
Kufikia sasa, nchi 11 zimechapisha rasmi kanuni za usanifishaji wa mbegu za COMESA kwenye magazeti yake rasmi ya serikali, zikiwemo Kenya, Uganda, Zambia, Ethiopia, Rwanda, Malawi, Burundi, Zimbabwe, Tunisia, Misri, na Eswatini.
Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC) inatarajiwa kujiunga mnamo Mei mwaka huu, 2025.
Viwango vya Utekelezaji (SOPs) chini ya COMSHIP, vimeandaliwa kwa mazao 13 yakiwemo mahindi, maharagwe, ngano, mtama, muhogo, viazi, njugu karanga, alizeti, pamba, soya, mchele na wimbi.
Nchini Kenya, taasisi ya Mbegu na Ustawishaji wa Mimea Nchini (Kephis) inaongoza katika usimamizi wa usajili wa mbegu na utekelezaji wa viwango vya afya ya mimea.

Hata hivyo, usambazaji wa mbegu feki ungali kero hasa maeneo yanayokuzwa nafaka.
“Miaka michache iliyopita tulianzisha mfumo wa ufuatiliaji wa mbegu kwa kutumia stika maalum zenye alama za kukwaruza ili kuthibitisha uhalisia wa mbegu,” akasema Joyce Karanja, Afisa Mkuu Mtendaji wa Muungano wa Wafanyabiashara wa Mbegu Nchini (STAK).
STAK, ni muungano ulioleta pamoja kampuni na mashirika yanayounda na kuuza mbegu kutoka kwa sekta ya umma na kibinafsi, shabaha yake ikiwa ni kuhamasisha sera bora.