Makala

Amerika yawekelea zawadi ya Sh1.2bilioni kwa kichwa cha Mojtaba Khamenei

Na BENSON MATHEKA, MASHIRIKA March 15th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

Katika juhudi za kuangamiza utawala wa urithi nchini Iran Amerika imetangaza zawadi ya hadi dola milioni 10 (Sh1.2 bilioni) kwa yeyote atakayetoa habari kuhusu maafisa wakuu wa jeshi na ujasusi wa Iran, akiwemo kiongozi wake mpya, Ayatollah Mojtaba Khamenei.

Haya yanajiri licha ya Rais Donald Trump kudai kuwa maafisa wa kijeshi wa Iran waligailiwa wakati wa shambulizi lililomuua Ayatollah Ali Khamenei, babake Mojtaba.

Zawadi hiyo inalenga maafisa 10 wanaohusishwa na Kikosi cha Walinzi wa Mapinduzi ya Kiislamu cha Iran (IRGC), kulingana na taarifa iliyochapishwa kwenye tovuti ya Wizara ya Masuala ya Kigeni ya Amerika.

Kikosi hicho cha kijeshi kilianzishwa baada ya Mapinduzi ya Kiislamu ya Iran ya mwaka 1979. Kinaaminika kuwa mwaminifu kwa kiongozi mkuu wa nchi na kimepewa jukumu la kulinda mfumo wa viongozi wa kidini wa Kishia.

Mojtaba Khamenei alimrithi babake, Ali Khamenei, kama kiongozi mkuu wa Iran aliyeuawa pamoja na maafisa wengine wa ngazi ya juu wa Iran katika mashambulizi ya pamoja ya Amerika na Israel yaliyoanza Februari 28.

Mojtaba Khamenei , ambaye inaaminika alijeruhiwa katika mashambulizi hayo, hajaonekana hadharani tangu wakati huo, ingawa alitoa taarifa yake ya kwanza Alhamisi.

Mbali na kiongozi huyo mkuu, Amerika pia inatafuta habari kuhusu mkuu wa usalama wa Iran Ali Larijani, Waziri wa Ujasusi Esmail Khatib, Waziri wa Usalama wa Ndani Eskandar Momeni, pamoja na maafisa wawili wanaofanya kazi katika ofisi ya Khamenei.

Larijani alionekana Ijumaa katika video zilizothibitishwa na shirika la habari la Reuters akiwa pamoja na Rais Masoud Pezeshkian na Waziri wa Masuala ya Kigeni Abbas Araqchi wakihudhuria mkutano wa hadhara mjini Tehran, licha ya kauli ya Waziri wa Ulinzi wa Amerika Pete Hegseth kwamba viongozi wa Iran walikuwa “wakijificha kwa hofu” chini ya ardhi.

Tovuti hiyo ya zawadi pia imeorodhesha maafisa wengine wanne, wakiwemo kamanda wa IRGC na katibu wa baraza la ulinzi, lakini haijataja majina yao wala kuweka picha zao.