Akili MaliMakala

Anavyotumia mitandao ya kijamii kusaka soko la bidhaa

Na SAMMY WAWERU February 19th, 2025 Kusoma ni dakika: 1

KINYUME na vijana wengine ambao hutumia safu za kijamii kujivinjari, kwa mfanyabiashara mchanga Wambui Kiritu ni tofauti.

Mjasiriamali huyu ambaye huoka mikate, keki na vitafunwa, hutumia mitandao ya kijamii kusaka wanunuzi wa bidhaa zake.

Wambui ana upekee kwenye biashara yake, kwani hutumia ndizi zilizoiva kupindukia kama mojawapo ya viungo kuoka snaki.

Kwenye mahojiano na Akilimali, mwasisi huyu wa Bobo Bakes alidokeza kwamba hutumia majukwaa kama X (awali Twitter), Instagram na Tiktok kunogesha soko la bidhaa zake.

Wambui Kiritu, mwanzilishi Bobo Bakes akirembesha keki. PICHA|SAMMY WAWERU

“Kila ninapooka mikate, keki na vitafunwa, hupiga picha za kuzipakia kwenye akaunti zangu,” akasema.

Isitoshe, hujirekodi video wakati akiandaa bidhaa na zaidi ya yote kuchangamsha wafuasi wake – ambao pia ni wateja wake wakuu, kwa maigizo.

Wambui alianzisha Bobo Bakes 2020, mwaka ambao Kenya na ulimwengu ilikuwa ikihangaishwa na gonjwa la Covid-19.

Bidhaa zake, aghalabu hulenga familia zenye watoto.

“Hufurahia sana ninapoona watoto wakiridhia bidhaa nilizoandaa,” akasema.

Hutia nakshi keki kwa virembesho, zionekana maridadi ubunifu ambao huvutia wanunuzi na watoto.

Baadhi ya virembesho ambavyo Wambui Kiritu hutumia kutia keki nakshi ili kuvutia wanunuzi. PICHA|SAMMY WAWERU