Akili MaliMakala

Apu inayosaidia kupunguza upotevu wa chakula

Na SAMMY WAWERU February 19th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

SUALA la upotevu wa chakula nchini lingali kero kuu haswa kwenye mashamba na masoko.

Kulingana na Wizara ya Kilimo na takwimu za Umoja wa Mataifa (UN), Kenya hupoteza kati ya asilimia 20 hadi 40 ya mazao yake ya kilimo kila mwaka kutokana na hasara za baada ya mavuno.

Katika taifa ambalo mamilioni ya watu wanakabiliwa na uhaba wa chakula na baa la njaa, hali hii ni kinaya kikubwa: mashamba huzalisha, masoko hufurika mazao wakati wa mavuno, lakini sehemu kubwa ya chakula haifiki mezani.

Badala yake, mazao huozea shambani na kutupwa kwenye masoko, yakichangia kero ya njaa na mabadiliko ya tabianchi.

Chakula kinapoozea kwenye majaa ya taka, huzalisha gesi chafu kama vile methane na kaboni, ambazo ni chocheo la ongezeko la kiwango cha joto duniani.

Triza Mwaniki, mkurugenzi mwenza Lynt’s Ltd, kampuni inayochakata ndizi eneo la Kahawa West, Nairobi. Picha|Sammy Waweru

Hasara hutokea katika kila hatua, kuanzia shambani, wakati wa usafirishaji, kwenye masoko na katika sekta ya hoteli na maduka makubwa.

Wakulima wadogo, ndio huumia zaidi kwa sababu ya kukosa miundomsingi faafu kuhifadhi na kuchakata mazao kurefusha muda wa kudumu. Wakati wa mavuno mengi, bei hushuka ghafla na mabroka hutumia mwanya huo kuwakandamiza kwa bei duni.

Seraphin Wanjiku, mkulima wa ndizi za kupika, plantain kwa Kiingereza, maarufu kama Mkono wa Tembo kutoka Kirinyaga, anasema mwaka 2023 alipata hasara kubwa baada ya soko kufurika mazao.

“Kwa mwezi, nilikuwa navuna wastani wa kilo 300, lakini mazao mengi yalikuwa yakiharibika. Ndizi huharibika haraka,” anasema, akikumbuka hasara aliyokadiria.

Kevin Otiende akielezea jinsi Msossi App inavyosaidia kupunguza upotevu wa chakula. Picha|Sammy Waweru

Kuangazia kero hiyo, mojawapo ya suluhu ni uongezaji thamani.

Triza Mwaniki, mwanzilishi mwenza Lynt’s Limited, kampuni iliyoko Kahawa West, Nairobi huchakata ndizi za plantain, na anakiri uongezaji bidhaa thamani ndio suluhu ya upotevu wa chakula.

Huunda kripsi, hivyo kurefusha muda wa kuhifadhi hadi miezi sita. “Kati ya Januari na Aprili, wakulima hupoteza zaidi ya asilimia 50 ya mavuno ya ndizi,” anasikitika.

Kwa kuzichakata, kando na kuongeza muda wa kudumu anawapa wakulima afueni kwa malipo bora.

Triza Mwaniki akielezea Lynt’s Ltd inavyochakata ndizi na kushirikiana na Msossi App kufikisha bidhaa zake kwa wateja kwa bei nafuu. Picha|Sammy Waweru

Hata hivyo, licha ya uchakataji kuonekana kusaidia kuziba gapu hiyo changamoto ya upotevu wa chakula kwenye hoteli, mikahawa na maduka ya kijumla bado ipo.

Afisa mmoja wa duka la kijumla jijini Nairobi anasema hupoteza kati ya asilimia 5 na 12 ya bidhaa za vyakula kila mwezi, hasara inayogonga mamilioni ya pesa kwa mwaka.

Kuangazia mahangaiko hayo, mbunifu Kevin Otiende ameibuka na programu ya kidijitali inayorahisisha uuzaji wa chakula.

Ameanzisha apu inayojulikana kama Msossi, madhumuni yake yakiwa kuunganisha maduka ya kijumla, hoteli na mikahawa kwa wateja wa bidhaa za kula.

Kevin Otiende akielezea jinsi Msossi Food App hutoa huduma. Picha|Sammy Waweru

“Tunalenga chakula kinachopikwa kwa wingi na kukosa kuisha na pia bidhaa ambazo muda wake wa kuharibika unakaribia. Kinapunguzwa bei,” Otiende ambaye ni Afisa Mkuu Mtendaji wa Food app Msossi anasema.

Kupitia apu hiyo, wauzaji huorodhesha bidhaa zao jioni, na wateja huchagua na kulipia kwa njia ya simu, wakitumia pia huduma za usafirishaji kama vile Glovo.

“Hakuna ada ya usajili. Tunachukua ada (commission) ya asilimia 20 hadi 30 kwa kila mauzo,” Otiende akaambia Akilimali wakati wa mahojiano kwenye ofisi yake Jijini Nairobi.

Mandazi yaliyoandaliwa na mkahawa mmoja Nairobi yakiuzwa kupitia picha zilizopakiwa kwenye apu ya Msossi. Picha|Sammy Waweru

Kufikia sasa, zaidi ya wauzaji 50 na watumiaji 1,000 wamejiunga na safu hiyo. Aidha, huduma zinatolewa katika Kaunti ya Nairobi kabla kusambazwa kwa maeneo mengine ya nchi.

Nairobi ni miongoni mwa kaunti zilizoathirika pakubwa na utupaji wa mazao ya kilimo kwenye masoko na pia hotelini na kwenye mikahawa.

Msossi app inaiga mfumo wa kidijitali ambao tayari ni maarufu Barani Ulaya na nchini Amerika, ambapo chakula kisichoisha kwenye mikahawa huuzwa kwa bei nafuu badala ya kutupwa.

Kwa Triza Mwaniki, ambaye pia ni mshirika kwenye jukwaa hilo, ubunifu huo unaashiria hatua kubwa kuokoa chakula na mazao ya shambani.

Mandazi yaliyoandaliwa na mkahawa mmoja Nairobi yakiuzwa kupitia picha zilizopakiwa kwenye apu ya Msossi. Picha|Sammy Waweru