‘Cucu’ alivyonichochea kuingilia biashara ya ufugaji kuku
ANN Wambui, 33, alizaliwa na kulelewa jijini Nairobi, na alipokuwa mdogo, alivutiwa sana na namna nyanya yake alivyofuga kuku katika mtaa wa Huruma, kiungani mwa jiji.
Ingawa mama yake pia alifuga kuku kwa matumizi ya nyumbani, ni mbinu za nyanyake zilizomhamasisha kufuata nyayo zake – ila kwa njia ya kitaalamu.
“Nikiwa mtoto, nilikuwa na hamu ya kujua chakula kinatoka wapi—hasa bidhaa za kuku,” anasema.
“Kwa sababu ya uhaba wa nafasi mjini, kuku wa nyanya walikuwa wakilala hata chini ya vitanda vya wageni. Hali hiyo ilinivutia sana, nikatamani kuingilia ufugaji wa kuku japo kwa mbinu za kisasa,” anaongeza.

Ili kutimiza ndoto hiyo, Wambui alianza kujielimisha kupitia mtandao.
TikTok ilikuwa mojawapo ya majukwaa yaliyomfundisha, akagundua kuhusu Kenchic, kampuni tajika kwa uzalishaji bidhaa za kuku – ikiwemo kutoa mafunzo ya ufugaji.
Aidha, Kenchic huangua mayai na kusambazia wakulima vifaranga waliopewa chanjo, ikiwa ni pamoja na kuuza kuku waliokomaa, nyama na bidhaa za kuku zilizoongezwa thamani. “Nilijiunga na mafunzo yao na nilifahamu mengi,” anadokeza.
Kupitia Kenchic, alifahamu jambo muhimu ambalo nyanya yake hakuzingatia ni usalama wa afya ya kuku, ikiwa ni pamoja na kuwepo kwa vizimba bora, chakula sahihi, na kudhibiti magonjwa.
Mwaka 2024, Wambui na mume wake waliamua kuanzisha rasmi mradi wa kuku.

Waligeuza kipande cha ardhi cha mita 15 kwa 30 walichokuwa wakikuza mboga na tini ‘beetroot’ eneo la Joska, Kaunti ya Machakos. Ili kuufanikisha, walitumia mtaji wa Sh1.5 milioni walizokuwa wameweka kama akiba.
“Tulianza na vifaranga 1,500,” anafichua, ingawa anasikitika walipoteza kuku wapatao 60 kwa sababu ya mkanyagano.
“Mitandaoni, huwa na hamasisho linaloegemea upande mmoja pekee, changamoto kwenye kilimo na ufugaji huwa nadra kuelezwa. Mafunzo ya mara kwa mara ni muhimu sana kuangazia gapu hiyo,” anasisitiza.
Mwaka mmoja baadaye, anajivunia mradi wao kuwa na kuku 3,000, wa kutaga mayai (layers).
Kwa mgeni anayezuru boma lao, hukaribishwa na sauti na kelele za kuku.

“Ninaposikia sauti zao, najua wana afya njema. Huwa na furaha sana,” Wambui anasema.
Amekumbatia mfumo wa kisasa kufanya ufugaji – ndio matumizi ya vizimba vilivyoboreshwa hasa kwa sababu ya usalama wa mayai, ndiyo cages.
Kabla kuingia kwenye vizimba, lazima uvalie aproni, kandambili na uloweshe makanyagio kwenye maji yaliyowekwa dawa kuua viini. Kanuni hiyo ‘biosecurity’ inalenga kuzuia kusambazia kuku maradhi kutoka nje.
Sheria hiyo, Wambui ameitilia mkazo pamoja na kigezo cha ufuatiliaji wa asili ya vifaranga na bidhaa.
Huweka rekodi za kina kuhusu maji, chakula, uzalishaji, afya, na chanjo.

Kulingana na Philip Maina, Afisa Mkuu wa Kibiashara Kenchic kanuni za biosecurity zinasaidia kuzuia watu kuingia kwenye makazi au makao ya kuku, ikiwa ni pamoja na kujumuisha usafi wa vifaa vya kula na maji, kutenga kuku wagonjwa au wapya, na kudhibiti wadudu na ‘adui’ kama vile panya na nyuni.
Kampuni hiyo pia ina programu za kidijitali na mtandao wa WhatsApp chatbot, inayosaidia wakulima kupata ushauri kwa wakati ufaao.
“Vifaranga wanapaswa kununuliwa kutoka kwa wasambazaji wa kuaminika na waliowachanja,” Maina anahimiza.
Wambui anasema huwa makini sana kwa vifaranga, hasa wakati wa kuwaotesha – brooding, ili kudhibiti baridi na kiwango cha joto
Ana mfanyakazi anayemsaidia kulisha kuku, kusafisha mabanda, na kukusanya kinyesi ambacho hutumia kulima mseto wa mboga kwenye bustani yake.

Mayai hukusanywa alasiri, na kwa sasa hukusanya wastani wa trei 45 kwa siku, na kuuzia wateja Nairobi, Machakos, na Kajiado.
Juni 7, ulimwengu uliadhimisha Sikukuu ya Usalama wa Chakula Duniani 2025, na Wambui anasisitiza haja ya ufuatiliaji kuku na bidhaa zake ili kuhakikisha uwepo wa bidhaa salama kwa walaji.
“Kuhakikisha mayai yanategewa eneo safi na yenyewe ni safi, chakula bora, usafi wa vibanda, na chanjo za mara kwa mara ndizo siri zangu kufanikisha biashara ya kuku,” akaambia Akilimali wakati wa mahojiano.
Ingawa changamoto kuu ni gharama ya chakula cha kuku, Wambui alisema kamwe hatakata tamaa.
Anajivunia kuwa kielelezo kwa mfanyakazi wake na pia mpwa wake, anaofichua kwamba tayari wameingilia ufugaji wa kuku kujiendeleza kimaisha.
