Makala

Edung- Mahasla ndio walinitia shime kuomba kazi ya mwenyekiti wa IEBC

Na CHARLES WASONGA May 31st, 2025 Kusoma ni dakika: 2

MWENYEKITI mteule wa Tume Huru ya Uchaguzi na Mipaka (IEBC) Erustus Ethekon Edung amefichua kuwa alitiwa shime na mahasla kuwasilisha ombi kwa wadhifa huo.

Akijibu maswali alipofika mbele ya Kamati ya Bunge la Kitaifa kuhusu Sheria na Masuala ya Kikatiba (JLAC) katika majengo ya Bunge, Jumamosi Mei 31, 2025, Bw Edung alifichua kuwa wahudumu wa kituo cha huduma za tarakilishi; Peter, Purity na Kizito ndio walimpa moyo kujitosa kwenye kinyang’anyiro cha cha kujaza nafasi hiyo.

“Awali, sikutaka kuomba kazi hii kutokana na mikosi mingi ambayo imewaandama washikilizi wa zamani wa kiti hiki. Lakini Wakenya hawa walinipa ujasiri na moyo wakisema ninahitimu kuwahudumia Wakenya katika cheo hiki. Na hivyo, ndivyo niliandaa stakabadhi zangu za maombi na nikawapa watayarishe na watume kisha nikaondoka kuelekea Afrika Kusini ninakofanya katika Shirika la Maendeleo la Umoja wa Afrika,” Bw Edung akaeleza wanachama wa kamati hiyo wakiongozwa na mwenyekiti wao George Gitonga Murugara.

Mwenyekiti huyo mteule, ambaye amewahi kuhudumu kama Mkuu wa Kitengo cha Sheria katika kaunti ya Turkana, aliwahakikishia wanachama wa JLAC kwamba atafanyakazi yake bila mapendeleo endapo uteuzi wake utaidhinishwa.

Bw Edung alihudumu katika kaunti ya Turkana kwa miaka minne, chini uongozi Josephat Nanok kama Gavana na kwa miaka miwili chini ya Gavana wa sasa Jeremiah Lomorukai.

Alikuwa akijibu malalamishi yaliyowasilishwa na mwanaharakati wa kutetea haki Dkt Magare Gikenyi akidai kuwa Bw Edung ni mwandani wa karibu wa Bw Nanok, ambaye sasa anahudumu kama Naibu Mkuu wa Wafanyakazi katika Ikulu ya Rais.

Ni kwa misingi hiyo ambapo, kulingana na Dkt Gikenyi, ambaye ni mkazi wa Nakuru, Bw Edung atampendelea Rais Ruto katika uchaguzi mkuu wa 2027 na hivyo wabunge wanapasa kukatalia mbali uteuzi wake.

Lakini Bw Edung akasema: “Ningependa kuihakikishia kamati hii kama uhusiano wangu na Mheshimiwa Nanok ulikuwa wa kikazi pekee. Nilishirikiana naye kuwahudumia watu wa kaunti ya Turkana na sio kwa misingi ya maswala mengine.”

Mwenyekiti huyo mteule wa IEBC, ambaye thamani ya utajiri wake ni Sh277,882,237, pia aliiambia Kamati ya JLAC kwamba yeye siye mwanachama wa chama chochote cha kisiasa.

Endapo JLAC itaidhinisha uteuzi wake, Bw Edung atajaza nafasi iliyoachwa wazi na aliyekuwa mwenyekiti wa IEBC marehemu Wafula Chebukati.