UCHANGANUZI: Mtego wa kutoka jadi unaovunja upinzani ufikapo uchaguzi mkuu
KUGAWANYIKA kwa upinzani si jambo geni katika siasa za Kenya.
Mwaka 1992, chama cha FORD kilichokuwa kimeibuka kama tishio kubwa kwa utawala wa KANU kilisambaratika baada ya viongozi wake Kenneth Matiba na Jaramogi Oginga Odinga kutofautiana kuhusu nani angewania urais.
Kutoka kwa mgawanyiko huo vilizaliwa vyama vya FORD-Asili chini ya Matiba na FORD-Kenya chini ya Jaramogi.
Badala ya kupambana na Rais Daniel arap Moi, viongozi hao waligeukiana, kila mmoja akidai ndiye aliyekuwa na haki ya kupeperusha bendera ya upinzani.
Zaidi ya miaka 30 baadaye, hali kama hiyo inaonekana kujitokeza tena.
Viongozi wa upinzani wanakubaliana kuwa Rais William Ruto anapaswa kukabiliwa na mgombea mmoja mwaka 2027. Hata hivyo, bado hawajakubaliana ni nani atakayebeba bendera hiyo.
Muungano unaowaleta pamoja Rigathi Gachagua, Kalonzo Musyoka, Fred Matiang’i, Martha Karua, Eugene Wamalwa na Justin Muturi unasema unataka mgombea mmoja.
Lakini kila upande unaonekana kutaka mgombea huyo atoke katika kambi yake.
Wakati huo huo, kiongozi wa Safina Jimi Wanjigi ameendelea na mkakati wake tofauti.
Kama alivyofanya Mwai Kibaki mwaka 1992, Wanjigi amesema atazingatia ajenda ya uchumi badala ya kujiingiza katika mvutano kuhusu nani anafaa kuongoza muungano.
Kwa sasa, wafuasi wa upinzani hawaonekani tu kumpinga Rais Ruto, bali pia wanapambana wao kwa wao.
Kila kambi inatumia matokeo ya kura za maoni na nguvu za maeneo yao kama ushahidi wa kwa nini mgombea wao anastahili kupewa tiketi.
Historia ya FORD inaonyesha hatari iliyopo. Kwanza, KANU haikuiangusha FORD. FORD ilianguka kwa sababu ya migawanyiko yake yenyewe.
Katika harakati za kutafuta mgombea bora, upinzani wa sasa unaweza kujikuta ukijenga migawanyiko itakayompa Ruto nafasi ya kushinda.
Wakati FORD ilipoanzishwa, ilionekana kama serikali inayosubiri kuingia madarakani.
Mikutano yake ilivutia umati mkubwa na viongozi wake waliheshimiwa kwa mchango wao katika mapambano ya kurejesha mfumo wa vyama vingi.
Lakini chama hicho hakikuwahi kuafikiana kuhusu namna ya kumpata mgombea wake wa urais.
Matokeo yake yalionekana wazi katika uchaguzi wa mwaka 1992.
Upinzani uliingia uchaguzini ukiwa umegawanyika kati ya Matiba, Jaramogi na Kibaki. Moi aliibuka mshindi huku kura za upinzani zikigawanyika.
Hilo lilichelewesha kuondolewa kwa KANU madarakani kwa takriban muongo mmoja.
Leo, viongozi wa upinzani wanakabiliwa na mtihani kama huo.
Gachagua amesema mgombeaji anaweza kutangazwa hata Mei 2027, ilhali Muturi ametaka uamuzi ufanywe mapema na tayari ameonyesha kumuunga mkono Kalonzo.
Martha Karua pia amehoji mfumo unaopendekezwa wa kumpata mgombeaji.
Wachambuzi wanasema miungano mingi haisambaratiki siku ya uchaguzi.
Huvunjika mapema kila upande unapoanza kujijengea mtandao wake, kukusanya fedha na kuwashawishi wafuasi kuwa hakuna mgombeaji mwingine anayefaa.
Hapo ndipo kinachoitwa athari ya Matiba huanza. Kila mwanasiasa anakubali umuhimu wa umoja, lakini kwa sharti kwamba umoja huo umuunge mkono yeye.
Somo jingine muhimu ni kwamba sheria na taratibu zinapaswa kuwekwa kabla ya majina ya wagombeaji.
FORD haikuwahi kukubaliana kuhusu mfumo wa kumpata mgombeaji wake, jambo lililochochea mzozo ulioigawa.
Kwa upinzani wa sasa, bado hakuna makubaliano kuhusu sifa za mgombeaji, ratiba ya uteuzi wala mfumo wa kutatua migogoro.
Historia pia inaonyesha kuwa umati mkubwa wa watu kwenye mikutano si lazima uwe ishara ya ushindi.
Matiba aliporejea nchini mwaka 1992 na kupokelewa na maelfu ya watu, wengi waliamini alikuwa tayari ameshinda. Lakini mvutano kuhusu mgombeaji ndio uliovunja FORD.
Aidha, muungano wowote unaotegemea tu kumpinga aliye madarakani huwa katika hatari ya kusambaratika. Swali ambalo Safina amekuwa ikiuliza ni: Baada ya Ruto, nini kitafuata?
Kwa mujibu wa Wanjigi, upinzani unapaswa kueleza sera zake kuhusu ushuru, deni la taifa, ukosefu wa ajira, ufisadi, afya, elimu na gharama ya maisha badala ya kutegemea kaulimbiu ya “Wantam” pekee.
Somo la mwisho ni kwamba umoja wa kweli huhitaji viongozi wengine kujinyima kwa manufaa ya lengo la pamoja.
Hilo lilitokea mwaka 2002, Raila Odinga alipomuunga mkono Mwai Kibaki kwa kauli maarufu ya “Kibaki tosha”, hatua iliyosaidia kuondoa KANU madarakani.
Historia ya FORD si simulizi ya zamani tu. Ni onyo kwamba upinzani unaweza kuwa na uungwaji mkono mkubwa wa wananchi, lakini ukashindwa ikiwa viongozi wake watashindwa kuweka maslahi ya taifa mbele ya tamaa zao binafsi.
Tatizo jingine ambalo lilichangia kusambaratika kwa FORD ni kwamba kila kiongozi aliamini historia yake ya kisiasa ilimpa haki ya kuwania urais.
Jaramogi alijiona ndiye aliyekuwa amepigania demokrasia kwa miongo mingi dhidi ya tawala za Jomo Kenyatta na Daniel arap Moi.
Kwa upande wake, Matiba aliamini mateso aliyopitia, ikiwa ni pamoja na kuzuiliwa bila kesi na kuugua kiharusi akiwa kizuizini, yalikuwa yamemjengea uhalali wa kuongoza upinzani.
Kila mmoja alitumia historia yake kama msingi wa kudai tiketi ya urais.
Hali kama hiyo inaonekana kujitokeza katika upinzani wa sasa.
Baadhi ya viongozi wanategemea ukongwe wao kisiasa, wengine wanajivunia idadi ya wapiga kura kutoka maeneo yao, huku wengine wakisisitiza tajriba yao serikalini, uadilifu wao au mateso wanayodai kuyapata kutokana na kupambana na utawala uliopo.
Ingawa hoja hizo zinaweza kuwapa nguvu kisiasa, hazitoshi kuwapa haki ya moja kwa moja ya kupeperusha bendera ya muungano.
Kwa mujibu wa historia ya FORD, umoja wa kisiasa haujengwi kwa hoja za nani ameteseka zaidi au nani anaungwa mkono na watu wengi zaidi, bali kwa kuweka utaratibu unaokubalika na wote.
Bila makubaliano ya wazi kuhusu namna ya kumpata mgombeaji na jinsi ya kushughulikia malalamishi yatakayojitokeza, tofauti za viongozi zinaweza kugeuka chanzo cha mgawanyiko na kuudhoofisha upinzani kabla hata ya kampeni rasmi kuanza.