‘Upanga’ wenye makali unaokata ODM, UDA
Hatua za vyama vya kisiasa kuwaondoa au kusukuma pembeni viongozi wenye ushawishi zimeanza kuonekana kama upanga wenye makali kuwili, huku wataalamu wakionya kuwa mara nyingi huleta matokeo kinyume na yaliyokusudiwa.
Aliyekuwa gavana wa Makueni, Profesa Kivutha Kibwana, anaeleza kuwa siasa za kuwaengua viongozi wakuu mara nyingi hujigeuza kuwa makosa ya gharama kubwa kwa vyama husika.
Akizungumza katika mahojiano ya runinga moja mnamo Alhamisi, Kibwana alifananisha kuondolewa kwa Naibu Rais Rigathi Gachagua na hatua za ndani ya ODM dhidi ya Katibu Mkuu Edwin Sifuna, akisema zote zinaonyesha mkondo mmoja wa kisiasa wenye madhara ya muda mrefu.
Profesa Kibwana anaamini kuwa kumtimua kiongozi mwenye nguvu si mwisho wake kisiasa, bali humjengea umaarufu zaidi. Kwa mujibu wake, hatua ya kumwondoa Gachagua ilimpa nafasi ya kujijenga kisiasa nje ya serikali na hata kupata uungwaji mkono mkubwa zaidi kutoka kwa wafuasi wake.
“Ikiwa ningekuwa Gachagua, ningesema aliyetimua alinifanyia wema kwa kunifanya kuwa maarufu zaidi kisiasa,” alisema Kibwana, akisisitiza kuwa mara nyingi wanasiasa wanaoondolewa huonekana kama waathiriwa na hivyo kuvutia huruma ya umma.
Mtazamo huu unaungwa mkono na mchambuzi wa siasa Macharia Munene, ambaye anasema kuwa hatua ya kumuondoa Gachagua haikuzingatia athari zake za baadaye. Akizungumza katika mahojiano ya runinga.
“Ilidhaniwa kwamba kumwondoa madarakani kungemaliza kabisa kisiasa, lakini badala yake ameibuka kuwa changamoto kubwa zaidi nje ya serikali. Ilionekana angeisha kisiasa, lakini amekataa kuisha na sasa ni tatizo kubwa zaidi kuliko vile angekuwa akiwa ndani ya serikali.”
Kwa mujibu wake, kumwacha kiongozi mwenye ushawishi nje ya mfumo wa serikali humpa uhuru wa kuikosoa bila mipaka, hali inayoweza kudhoofisha uongozi uliopo. Aidha, alibainisha kuwa umaarufu wa Gachagua umeongezeka hasa katika eneo la Mlima Kenya, ambako anaendelea kujipatia uungwaji mkono mkubwa.
Munene aliongeza kuwa: “Ilikuwa salama zaidi kumdumisha ndani ya serikali kuliko kumtimua, kwa sababu ana mengi anayoyajua na anaweza kuzungumza bila woga, jambo linaloleta presha kwa uongozi uliopo.”
Ndani ya vyama vya kisiasa, hali kama hiyo pia imeonekana. Profa Kibwana alitaja hatua ya ODM dhidi ya Edwin Sifuna kama mfano mwingine wa jinsi vyama vinavyoweza kujikosea kwa kuwasukuma nje viongozi wao wenye mvuto kwa umma. Anaonya kuwa hatua kama hizo huongeza hadhi ya viongozi hao badala ya kuwapunguza nguvu.
Sifuna alivuliwa wadhifa wa katibu mkuu wa ODM kisha akazindua vuguvugu la Linda Mwananchi ambalo limekuwa likivutia umati kila linapoandaa mikutano hasa vijana ambao ndio wapiga kura wengi. Leo, kundi hilo linatarajiwa kuwa na mkutano wa hadhara kaunti ya Nakuru katika ngome ya kisiasa ya Rais William Ruto.
Kwa upande wa kisheria, Kibwana alieleza kuwa hatima ya Gachagua bado haijafungwa, kwani kesi zake bado ziko mahakamani na zinaweza kubadilisha mwelekeo wa siasa zake siku zijazo. Hii ina maana kuwa uwezekano wa kurejea kwake kisiasa bado upo wazi.
Wakati huo huo, Kibwana aliwashauri viongozi wa upinzani kujifunza kutokana na hali hiyo na kuandaa sera madhubuti badala ya kutegemea tu ukosoaji wa serikali. Alifananisha hali ya sasa na mwanzo wa muungano wa NARC miaka ya 2000, akisema kuwa ni wakati wa kupanga mikakati ya kisera kuelekea uchaguzi wa 2027.
Alisisitiza kuwa masuala kama ufisadi, utawala wa sheria na ukosefu wa ajira kwa vijana yanapaswa kuwa kiini cha ajenda ya kisiasa.
Wataalamu wanaafikiana kuwa vyama vinapaswa kuwa makini vinapochukua hatua dhidi ya viongozi wenye ushawishi. Japo vinaweza kuzima upinzani wa ndani, hatua hizo mara nyingi huimarisha hadhi ya wanaotimuliwa na kuwapa jukwaa jipya la kisiasa.
“Katika mazingira ya siasa za Kenya, ni wazi kuwa kuwaondoa viongozi hakumaanishi mwisho wao—bali huenda ikawa mwanzo wa safari mpya yenye nguvu zaidi kisiasa,” asema mchanganuzi wa siasa Dkt Isaac Gichuki.