Makala

Jinsi Ruto alivyowachezea wasanii

Na SINDA MATIKO June 12th, 2025 Kusoma ni dakika: 3

WAKATI wa kampeni ya kuelekea uchaguzi mkuu wa 2022, Rais William Ruto alisaka kura za wasanii kwa kutoa ahadi kadhaa za kuboresha maisha yao.

Kwenye mikutano yake kadhaa na wasanii wa fani mbalimbali, Dkt Ruto alitumia kauli “pesa mfukoni” na “Nikiweka Bibilia chini” kukariri jinsi angetekeleza ahadi hizo haraka.

Sasa ambapo utawala wake umedumu afisini kwa siku 1000 maswali yameibuliwa iwapo ametimiza ahadi hizo au la.

Kwa mfano, Dkt Ruto aliahidi kuleta mabadiliko ya kuimarisha sekta ya usanii, inayochangia asilimia 5.3 kwa Jumla ya Pato la Kitaifa (GDP).

Aliahidi kufanikisha hilo kwa kudhamini Mswada wa Sekta ya Ubunifu, kubuni Hazina ya Kitaifa ya Filamu na kuondoa aina mbalimbali za ushuru zinazotozwa watengeneza filamu.

Pia Rais Ruto aliahidi kujenga kumbi za michezo ya kuigiza ya za maonyesha ya sanaa na kuendeleza ujasiriamali kupitia muziki.

Kuhusu sekta ya filamu, alitoa ahadi kadhaa.

“Tutaanzisha mtindo wa kuanzishwa kwa leseni kwa wasanii wote. Tutaanza mpango wa kurahisisha uwezekano wa watengeneza filamu kutoka ng’ambo kuja nchini na kutoa nafasi kwa watengeneza filamu wa humu nchini kuuza filamu zao ng’ambo,” akaahidi mnamo Septemba 2022.

Swali ni je, wasanii wameanza kuhisi matunda ya utekelezaji wa ahadi hizo au wamevunjwa moyo.

Jennifer Ochieng, ambaye ni mtengeneza filamu maarufu na mwanzilishi wa “Sinema Focus” anasema sekta hiyo haijanufaika pakubwa chini ya uongozi wa Ruto.

Kwa mtazamo wake, licha ya sekta ya filamu kuzalisha Sh86.9 bilioni mnamo 2022, kulingana na ripoti iliyotayarishwa na Tume ya Filamu Nchini (KFC) na Shirika la Kitaifa la Takwimu (KNBS), sekta hiyo inaendeshwa bila sera na mipango ya kuiwezesha kupiga hatua kimaendeleo.

“Mnamo 2024 serikali ilitangaza kuwa ingeondoa ushuru na kuvumisha Kenya kama kituo bora za kutengenezea filamu ya hadhi ya Hollywood. Hatua kama hizo hazijachukuliwa kuwaondolea mzigo wa ushuru watengenezaji filamu wa humu nchini inavyofanyika nchini Afrika Kusini,” akaeleza Bi Ochieng’.

Kulingana na msanii huyo, hatua ya serikali kubadilisha mawaziri wanaosimamia sanaa kila mara inaashiria kuwa haina mpango madhubuti wa kuimarisha sekta hiyo.

Tangu Rais alipoingia mamlakani Idara hiyo imesimamiwa na mawaziri Ababu Namwamba, Kipchumba Murkomen na sasa Salim Mvurya.

Hata hivyo, Bi Ochieng’ anasema wakati wa hatamu ya Bw Namwamba, hatua kidogo ilipigwa katika kuimarisha sekta hiyo.

“Namwamba alileta matumaini kwamba mambo yangeenda vizuri. Aliongoza juhudi za ushirikiana kati ya watengenezaji filamu wa Kenya na wale wa ng’ambo. Alipigania kuanzishwa kwa Hazina ya Kitaifa ya Filani, kupunguzwa kwa ushuru, mageuzi ya kisera na vishawishi kama vile kupunguzwa kwa ada ya leseni kwa kima cha asilimia 15. Hata hivyo, juhudi hizo zilikwama alipoondoka. Baadaye kile tumeshuhudia ni serikali kujitia hamnazo kuhusu masilahi ya sekta hii ya sanaa,” akasema.

Roy Gitahi, ambaye ni mwanzilishi wa shirika la Art at Work and Wabuni Sacco anakubaliana na kauli za Bi Ochieng.

Anaamini kuwa serikali imekosa mwelekeo na haina nia ya kuinua sekta hiyo.

“Utawala unasema mengi na kutenda machache. Ni vigumu kujua ikiwa iko katika sekta ya umma au kibinafsi. Wajibu wa serikal ni kubuni mazingira bora ambako sekta ya kibinafsi inaweza kunawiri. Mbona serikali ya Rais Ruto inachukua majukumu ya sekta ya kibinafsi. Je, ni kwa sababu wanaofaidi wako ndani ya serikali?,” Bw Gitahi anauliza.

Anasema Rais mstaafu Uhuru Kenyatta alielewa sekta hiyo na ndio maana alibuni Jopo Kazi kuhusu Uchumi wa Usanii.

Jopokazi hilo lililenga kuboresha sekta hiyo ili iwe ya kutegemewa kama chanzo cha kitega uchumi kwa wasanii.

Lakini kulingana na Bw Gitahi juhudi hizo zimedumazwa baada ya Rais Ruto kuingia mamlakani.

“Hii ndio maana wakati huu wasanii hawawezi kupata mkopo kutoka kwa benki kwa kutumia kazi zao kama dhamana, hali ambayo imewafanya kuendelea kuishi kwa umasikini,” akaeleza.

Bw Gitahi anasema kuwa Ruto alipoingia mamlakani, nafasi ya jopo kazi hilo ilitwaliwa na Talanta Hela.

“Watu wanaoketi katika asasi hiyo hawaelewe mahitaji ya wasanii. Hawana uelewa wa masuala ya kifedha, sio wataalamu bali ni wanamitindo wasioelewa chochote,” anasema.