• Nairobi
  • Last Updated April 30th, 2024 6:55 PM
KINA CHA FIKIRA: Tumia ubora ulio nao kufanyia kazi bora ili ufanikiwe

KINA CHA FIKIRA: Tumia ubora ulio nao kufanyia kazi bora ili ufanikiwe

Na WALLAH BIN WALLAH

BINADAMU ana ubora wa kipekee.

Hawezi kupaa angani kama ndege wanaotumia mbawa zao kupaa angani. Lakini binadamu ana akili na ujuzi wa kutengeneza vyombo vinavyomsaidia kupaa kuenda mbali zaidi ya ndege wanaotumia mbawa!

Binadamu hawezi kuogelea au kupiga mbizi ndani ya maji kama samaki wanaotumia mapezi kuogelea na matamvua ya kuvutia hewa majini. Lakini binadamu anatumia akili na ubora wake kuunda vyombo vinavyomsafirisha katika maji baharini, maziwani na mitoni.

Binadamu hana macho makali ya kuona mbali kama ndege waitwao mwewe, kipanga na tai. Lakini ana uwezo wa kutazama na kuona vitu au mambo yanayotokea pande zote duniani kwa kutumia vyombo bora alivyovivumbua kama vile runinga, darubini na darumbili!

Binadamu hana uwezo wa kukimbia kasi kama duma, farasi, sungura na swara ardhini. Lakini ameunda magari ya kila aina yanayomsafirisha kwa mwendo kasi nchi kavu.

Binadamu amefaulu kuyatenda yote hayo kwa sababu ana uwezo wa kufikiri, kuvumbua na kubuni mbinu bora zaidi za kuishi katika mazingira yake duniani.

Masikitiko ni kwamba watu wengine hawafanyi jitihada kuutumia ubora na uwezo waliojaliwa na Mwenyezi Mungu angalau kufanya kazi au shughuli zao kubwa au ndogo zikawa bora! Aidha wapo watu wanaokubali kushindwa hata kabla hawajajaribu! Kushindwa kufanikiwa na kufaulu kufanikiwa ni uamuzi wa mtu binafsi! Ni unyonge mkubwa kutarajia kupata kitu chochote bila ya kutafuta au bila ya kutia bidii kwa matarajio kwamba Mwenyezi Mungu ataleta kila kitu!

Katika kijiji cha Jikazeni, kando ya barabara kuu inayoelekea mjini, kulikuwako mashamba mawili ya mahindi yaliyopakana. Yote yalikuwa na ukubwa sawasawa wa ekari mbili. Lakini shamba moja lilikuwa na mahindi yaliyostawi vizuri zaidi. Shamba jingine lilikuwa na mahindi hafifu yaliyosinyaa na kunyaukanyauka!

Profesa Sifatupu alikuwa akiliendesha gari lake kuelekea mjini. Alipoyaona mashamba yale, alishtuka akaliegesha gari pembezoni ili ayatazame vizuri! Akasema, “Mashamba haya yamelimwa katika mazingira yanayofanana! Lakini Mungu amelibariki shamba hili moja likastawisha mahindi vizuri sana!”

Kumbe mwenye shamba zuri, Bwana Mtukazi alikuwa shambani akilinda ndege wasimharibie mahindi! Alipoyasikia maneno ya Profesa Sifatupu, alitokeza akasema, “Naam! Ninakubali Mwenyezi Mungu amelibariki shamba langu! Ninashukuru! Lakini ujue kwamba nililima mapema, nikapanda mbegu vizuri, nikaweka mbolea na kupalilia vizuri! Angalia, wakati huu nipo hapa nikiwafukuza ndege wasile mahindi yangu!

Ndugu wapenzi, ukifanya kazi yako vizuri na kuitunza vyema, bila shaka Mwenyezi Mungu ataleta baraka!

[email protected]

You can share this post!

GWIJI WA WIKI: Jane Angila Obando

Sossion awataka wazazi wawe watulivu majadiliano kuhusu...