JIFUNZE LUGHA: Japo maneno ‘hata’ na ‘hadi’ ni visawe, ‘hadi’ halina maana ya ‘pia’
BINTI yangu anaponisalimu “umeshindaje?”, humtaaradhi ili kufahamu iwapo ameshinda vyema pia. Hivi ndivyo hunijibu: “Hadi mimi nimeshinda vyema”.
Matumizi ya neno ‘hadi’ katika itiko la binti yangu yanaibua taksiri ya kimaana. Kadiri nijaribuvyo kumwelekeza kuwa neno mwafaka linalopaswa kutumiwa kwa maana ya ‘pia’ ni ‘hata’ ndivyo alirudiavyo kosa hilo.
Nilikuwa nimefikia mkataa kuwa yamkini sauti /d/ hutamkwa kwa urahisi na watoto wa umri fulani kuliko /t/, nilipokumbana na kosa lilo hilo tena katika baadhi ya kazi za wanafunzi wa kiwango tofauti ambazo mimi huzisahihisha aghalabu.
Kwa mintarafu hii, nimegundua kuwa maneno ‘hadi’ na ‘hata’, japo yanaonekana kuwa ya msingi mno, huwakanganya baadhi ya watumizi wa lugha ya Kiswahili.
Kimsingi, matumizi yasiyofaa ya ‘hadi’ kwa maana ya ‘pia’ yamkini husababishwa na mambo kadhaa. Mojawapo ya mambo hayo ni ukuruba uliopo baina ya ‘hata’ na ‘hadi’ kimaana.
Katika baadhi ya kamusi za Kiswahili nilizozitazama, neno ‘hadi’ linaelezewa kuwa ni kisawe cha ‘hata’. Yaani, usemi ‘Utaendelea kuteseka hadi lini?’ – kwa mujibu wa kamusi hizo – una maana sawa na ‘Utaendelea kuteseka hata lini?’
Aidha, kauli, ‘Kutoka hapa hadi pale ni mita mia moja’ ina fasili sawa na ‘Kutoka hapa hata pale ni mita mia moja’.
Katika sehemu ya pili ya makala, nitafafanua kwa nini neno ‘hadi’ halipaswi kutumiwa kwa maana ya ‘pia’ licha ya usawe linaoshiriki na ‘hata’.
…YATAENDELEA
[email protected]