Lugha, Fasihi na Elimu

Matumizi ya mbinu rejeshi katika kuiendeleza riwaya ya ‘Nguu za Jadi’

Na JOYCE NEKESA, Kapsabet Boys February 25th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

JUMA hili tutashughulikia nafasi ya mbinu rejeshi katika riwaya. Hii ni mbinu ambayo mwandishi hurejelea matukio ya awali ili kutupatia msingi wa matukio ya wakati huo.

Hutumika mhusika anapokumbuka kitu au tukio la awali lililo na uhusiano fulani na tukio la wakati huo. Hutumika kujaza mapengo ya kimsuko ambayo yangekuwepo bila matukio hayo ya awali.

Mbinu hii huchangia katika kukuza maudhui, kuwatambulisha wahusika na sifa zao.

Pia huendeleza ploti na dhamira ya mwandishi. Baadhi ya migogoro hujitokeza ama kutatuliwa kupitia mbinu hii rejeshi. Kwa mfano:

Tunafahamu kuhusu kuteketezwa kwa makao ya Matango kupitia masimulizi ya Mangwasha amekimbilia usalama wake kanisani. (Ukatili)

Chanzo cha chuki kati ya jamii ya Wakule na Waketwa inajitokeza kwa njia rejeshi kwamba imekuwepo tangu jadi. (Uk.6-7). (Ukabila).

Tunajuzwa kuhusu Mrima kutelekeza familia yake kupitia mbinu rejeshi. Hali hii inamfanya Mangwasha kuwa na uchochole na mashaka mengi.

Mangwasha anapozidi kutaabika kwa kutelekezwa na mumewe anakumbuka mafunzo aliyopewa utotoni na wazazi wake, kwa mfano kuuambaa uvivu na kujihadhari na vitu vya kupewa pamoja na mafunzo mengine mengi yanayomfaa wakati huo. (Uk.12). (Malezi mema).

Maelezo kuhusu usuli wa Mangwasha pamoja na harusi yao na Mrima inajitokeza kupitia mbinu rejeshi. (Uk.14).

Mrima anakumbuka kumuona awali mwanamke aliyekuja kuivuruga arusi yao. Anasema kuwa alikuwa mwanamke aliyekuwa amewahi kutumwa na Sagilu kumletea barua afisini mwake wakati mmoja. (Uk.24).

Kupitia kwa mazungumzo ya Mangwasha na Mbungulu, tunagundua kuwa Mangwasha ni mjane na mumewe hakuwa mlevi. (Uk.33). (Uwajibikaji).

Tunatambua kuwa ubaguzi wa ajira kwa misingi ya ukabila nchini Matuo unakiuka ujadi wa nchi hiyo uliotambua ujuzi, maarifa na taaluma ya mtu kabla ya kupewa ajira. (Uk.47).

Mangwasha na wenziwe walikumbuka uchomaji wa makazi yao ulivyotekelezwa na vijana kwa msaada wa mwenye gari jekundu lililobainika baadaye kuwa lilikuwa la Sihaba. (Uk.67).

Mangwasha anapopata bahasha kubwa juu ya kabati inamkumbusha ile siku ambayo aliiona na Chifu Mshabaha afisini mwake. (Uk.105). (Ufisadi).

Tunatambua kuwa Cheiya ni yatima aliyelelewa katika makao ya mayatima, akasomeshwa na kufuzu chuoni kupitia mbinu rejeshi, baada ya kuchumbiana na Mashauri.

Tunarejeshwa nyuma kwa maisha ya awali ya Lonare mwanawe Lombo alipokuwa amerejea kutoka ughaibuni.

Tunatambua kuwa aliteseka kuwalea wanawe baada ya mkewe kufariki. (Uk.130).

Tunatambua kupitia mbinu hii kuwa babake Ngoswe ni Sagilu Nanzia anapomfahamisha akiwa hali mahututi hospitalini. (Uk.160).