Makala

Mauaji ya Ojwang: Konstebo Mukhwana kuendelea kukaa ndani

Na RICHARD MUNGUTI June 14th, 2025 Kusoma ni dakika: 2

AFISA wa Polisi James Mukhwana aliyekamatwa kwa tuhuma za kumuua mwalimu- bloga Albert Omondi Ojwang katika kituo cha Polisi cha Central atendelea kukaa rumande hadi Juni  20, 2025 mahakama itakapoamua ikiwa ataachiliwa kwa dhamana au la.

Konstebo Mukhwana aliyekamatwa Juni 12,2025 ndiye aliyekuwa na kifunguo cha seli ambapo Ojwang alikutwa ameaga na yaaminika anajua walioingia katika seli hiyo na kutekeleza mauaji hayo.

Afisa wa IPOA-Abdirahaman Jibril alimwelezahakimu mwandamizi wa mahakama ya Milimani Bw Robinson Ondieki kwamba polisi wanatumia mwongozo wa-Blue Code of Silence-BCS kuzika ukweli kuhusu mauaji hayo ya kinyama ya Ojwang.

Mauaji ya Ojwang yamezua hisia kali katika nyanja mbali mbali na pia kuzua vurugu kali na maandamano hata kujadiliwa na mabunge ya Seneti na Bunge la Kitaifa.

Vile vile hakimu alielezwa na Jibril kwamba Rais William Ruto amezungumzia suala hilo na kuahidi waliohusika na mauaji ya mwalimu Ojwang watachukuliwa hatua kali za kisheria.

Akiwasilisha ombi la Konstebo James Mukhwana azuiliwe kwa siku 21 Bw Jibril alisema afisa huyo ndiye alikuwa na kifunguo cha seli alimofungiwa Ojwang.

Jibril aliemweleza Bw Ondieki, Ojwang alifikishwa kituo cha Central mnamo Juni 7,2025 baada ya kukamatwa na maafisa sita wa uchunguzi wa jinai (DCI) kutoka nyumbani kwake kaunti ya Homa Bay.

Keshoye Juni 8,2025 Ojwang alikutwa amekufa ndani ya seli “huku kidimbwi cha damu kimemzunguka.”

Bw Jibril alisema Ojwang aliondolewa na kupelekwa Hospitali ya Mbagathi alipothibitishwa ameaga.

Kichwa na mwili ulikuwa na majeraha na uchunguzi wa mpasuaji rasmi wa Serikali ulionyesha Ojwang aliteswa kabla ya kuuawa.

Konstebo Mukhwana alitiwa nguvuni Juni 12,2025 na kuzuiliwa katika kituo cha polisi cha Capitol Hill kuhojiwa.

Mahakama iliambiwa washukiwa wengine ambao ni maafisa wa polisi wametoroka na wanaendelea kusakwa.

“Mukhwana ndiye mshukiwa mkuu kwa vile ndiye alikuwa na kifunguo cha seli ambapo Ojwang alifungiwa kabla ya kupatikana ameaga,” Bw Jibril aliambia polisi.

Bw Ondieki alifahamishwa kamera za CCTV katika kituo hicho cha polisi ziliharibiwa usiku wa Juni 7,2025.

Bw Jibril alipinga Konstebo Mukhwana akiachiliwa kwa dhamana akisema atavuruga ushahidi na ukweli kuhusu mauaji ya kinyama ya Ojwang hautawahi julikana.

Hakimu aliambiwa mipango jinsi Ojwang atavyokamatwa na kuuawa ilipangwa na maafisa wakuu katika idara ya polisi.

“Konstebo Mukhwana yuko na habari muhimu zitakazopelekea kutiwa nguvuni kwa waliomuua Ojwang,” Bw Jibril alisema.

Mahakama ilielezwa kwamba kuna njama za kuficha ukweli kuhusu mauaji ya kinyama ya Ojwang ambayo yamesababisha maandamano na shutuma kali dhidi ya wakuu katika idara polisi.

“Polisi wakuu pamoja na wale wa ngazi za chini wameamua kutumia mwongozo wa polisi almaarufu Blue Code Silence (BSC) kuficha ukweli kuhusu mauaji hayo ya Mwalimu Ojwang,” Bw Jibril alidokeza.

Alisema wataalam wa masuala ya kitechnolojia tayari wametwaa simu ya Konstebo Mukhwana kuichunguza.

Mahakama ilifahamishwa Mukhwana amekuwa akiwasiliana na wahusika katika mauaji ya Ojwang.

Mawakili Danstan Omari na Stanley Kinyanjui waliomba  Mukhwana aachiliwe kwa dhamana wakisema “hakuna sababu maalum zilizowasilishwa na upande wa mashtaka kuwezesha mahakama imnyime dhamana.”

Bw Omari aliomba mahakama imwachilie Ojwang kwa dhamana na kumwagiza asiende karibu na kituo cha polisi cha Central.

Bw Omari alisema Mukhwaana alitiwa nguvuni baada ya wananchi kuchemka kwa hasira huku viongozi wa tambaka mbali mbali akiwamo Rais Ruto kuzugumzia kwa uzito suala hilo la kuuawa kwa Mwalimu Ojwang.

Baada ya mawasilisho ya upande wa mashtaka na Bw Omari mahakama iliamuru Mukhwana azuiliwe katika kituo cha polisi cha Capitol hadi Juni 20,2025 atakapojua ikiwa ataachiliwa kwa dhamana au la.