• Nairobi
  • Last Updated May 2nd, 2024 7:50 AM
MAWAIDHA YA KIISLAMU: Katazo la mtu kukaa chemba na mwanamke asiye maharimu wake

MAWAIDHA YA KIISLAMU: Katazo la mtu kukaa chemba na mwanamke asiye maharimu wake

Na HAWA ALI

SIFA zote njema anastahiki Mola Azzawajalla, Mwenye kuneemesha neema kubwa kubwa na nyingine ndogondogo.

Swala na salamu zimwendee Mtume wetu Muhammad SAW Maswahaba wake kiram na watangu wema hadi siku ya malipo.

Kisheria kijana wa kiume anaruhusiwa kumuangalia mtoto wa kike uso na mikono anapotaka kumposa bila ya kumgusa na hili hufanyika mbele ya wazazi wa pande zote mbili.

Hekima ya mkutano huu na kuonana huku ni kuwapa vijana hawa fursa ya kumuona yule atakayekuwa mwenza wake katika maisha na pia kuamua kukubali kuoa au kuolewa ama kukataa. Hili tu ndilo linaloruhusiwa na sheria.

Baada ya kuonana huku, wachumba hawa hawana ruhusa ya kuzungumza au kuonana tena mpaka watakapooana kwa misingi na taratibu zote za kisheria ambapo binti sasa hutambulika kama mke wa mtu na kijana kama mume wa mtu.

Yaliyozuliwa na watu kinyume na utaratibu huu tuliowekewa na sheria ni HARAMU isiyokubalika na yenye adhabu kali mbele ya Mwenyezi Mungu Mtukufu kutokana na athari yake mbaya kwa jamii.

Uzoefu umeonyesha na kuthibitisha kuwa ada hii ya “kuzoeana kitabia” katika hatua ya uchumba imefanya ndoa nyingi zisifungwe.

Kijana wa kiume akishapata nafasi ya kukutana na binti na kufanya tendo la kuonana kimwili kabla ya ndoa, matokeo yake ni kumtia mimba mtoto wa kike. Baada ya mimba hupatikana mojawapo ya mambo mawili haya:

Ama kijana ataukubali mzigo wake ule, akalea mimba na wakaja kufunga ndoa baadaye wakiwa na mtoto wa haramu/nje ya ndoa.

Au ataukana mzigo ule kuwa si wake na hivyo kumuacha mtoto wa kike ahangaike na kuteseka peke yake naye akashika nia kwenda kuendeleza fisadi na uharibifu wake kwingineko.

‘Kwa maslahi yetu’

Sasa ili kuzuia haya yote yasitokee, ndio Uislamu ukaamua kuufunga kabisa mlango huu wa fisadi na uharibifu kwa maslahi yetu wenyewe.

Tufuatane pamoja katika hadithi ifuatayo ya Bwana Mtume, ili tuone jinsi Uislamu ulivyoharamisha mwanamume kumuangalia mwanamke ajnabia (wa kando na kando – yaani si maharimu wa mwanamume yule):-

Imepokelewa na Umu Salamah – Allah amuwie radhi – amesema: Nillikuwa mbele ya Mtume wa Mwenyezi Mungu – Rehema na Amani zimshukie – akiwa na Maimunah (mkewe), akaja/akaingia Abdullah Ibn Ummi Maktuum (kipofu).

Na hili lilikuwa baada ya kushuka aya za hijabu, akatuambia Mtume; “Jificheni nae,” tukamwambia; Ewe Mtume wa Mwenyezi Mungu, je, yeye si kipofu? Hatuoni na wala hatujui ? Mtume akatuambia; “Je! Na nyinyi ni vipofu, hamumuoni ?” Abuu Daawoud na Tirmidhiy.

Haya, ikiwa huyu ni kipofu haoni na bado Bwana Mtume anawaamrisha wakeze waondoke mbele yake, wasimuone kwa kuwa ni mwanamume.

Vipi leo, vijana wetu wa kike na wa kiume ambao wote wawilli si vipofu wanaona wakae pamoja wakitazamana na kuzungumza kwa tabasamu pevu na vicheko vya furaha?

Ruhusa hii na uhalali huu wanaupata wapi na ilhali Bwana Mtume – Rehema na Amani zimshukie – anatuonya:

“Asikae faragha mmoja wenu pamoja na mwanamke ila (atakapokuwa mwanamke huyo) pamoja na maharimu wake.” Bukhaary na Muslim.

Bwana Mtume, anatukataza katika hadithi hii kukaa faraghani (yaani mwanamume na mwanamke peke yao tu) pamoja na mwanamke ambaye si maharimu yetu.

Mwanamke asiye maharimu ni yule ambaye kisheria hakuna kizuizi wala kipingamizi chochote kwetu kumuoa.

Haya ni maelekezo, maagizo na amri ya Bwana Mtume ambayo sisi kama Waislamu tunapaswa bali imetulazimu na kutuwajibikia kuifuata na kiutekeleza mara moja bila ya kuzitii na kuzifuata amri na maelekezo ya Bwana Mtume – Rehema na Amani zimshukie.

Na ni vema ikatiwa akilini kuwa kumtii na kumfuata Bwana Mtume ni amri ya mwenyezi Mungu Mtukufu, tusome na tutekeleze.

“… Na anachokupeni Mtume (anachokuamrisheni basi pokeeni), na anachokukatazeni jiepusheni nacho.” (59:7)

Tusome tena kwa mazingatio na kisha tufuate:

“Sema: Ikiwa nyinyi mnampenda Allah, basi nifuateni; (hapo) Allah atakupendeni na kukughufirieni madhambi yenu.” (3: 31)

Aya hizi na nyinginezo ndizo zinazotulazimisha kumfuata na kumtii Bwana Mtume katika maelekezo, maamrisho au makatazo yote atakayotupa kwa maslahi na manufaa yetu wenyewe.

Kwa bahati nzuri Mwenyezi Mungu Mtukufu ametukamilishia dini hii kupitia kwa Mtume wake.

Dini hii haikusaza lolote lenye manufaa na faida kwetu katika maisha haya ya dunia na yale yajayo ya ahera ila imetueleza jambo hilo na namna ya kulitekeleza.

Kadhalika haikuacha lolote lile lenye madhara na kasoro kwetu ila imetubainishia na kututahadharisha nalo na kutuonya tusilitende au kulifuata.

Sasa ikiwa dini hii imekamilika na kila jambo linalohusu nyanja mbalimbali za maisha yetu ya kila siku limekwisha bainishwa na kuwekewa utaratibu wake wa kulitekeleza au kulienda.

Kwenda kinyume na utaratibu huo, kunamaanisha:

Dini hii haikukamilika kama anyavyosema Mwenyezi Mungu Mtukufu.

Kumkadhibisha Mwenyezi Mungu na Mtume wake, jambo ambalo ni maasi.

Sisi tunayo mamlaka na madaraka ya kujitungia sheria kinyume na sheria za Mwenyezi Mungu Mtukufu.

Tuna uamuzi na hiari ya kufuata ama kutokufuata sheria/ hukumu za Mwenyezi Mungu Mtukufu.

Sheria na taratibu zetu tulizojipangia ni bora na zinafaa zaidi kuliko zile za Mwenyezi Mungu.

Kumpinga Mwenyezi Mungu na Mtume wake.

Kwa ujumla kutokumfuata Bwana Mtume ni kumhalifu na kumpinga, jambo ambalo Mwenyezi Mungu mtukufu ametukataza tusome na tuzingatie:

“ … Basi wajihadhari wale wanaokaidi amri yake wasije wakapata msiba au ikawafika adhabu iumizayo…” (24: 63)

Leo kwa sababu ya ukaidi na kukhalifu kwetu amri ya Bwana Mtume – Rehema na amani zimshukie – na tukaruhusu mila na desturi hii ya kuzoeana tabia iitawale jamii yetu – tayari tumeshafikwa na kupatwa na msiba.

Msiba huu si mwingine bali ni wimbi na janga la watoto wa haramu/nje ya ndoa na pengine hata hawa tuwaitao leo watoto wa mitaani ni natija ya kuendekeza na kufuata mila tamaduni na desturi hizi mbaya.

Taathira na athari na ada hizi potofu ziko wazi na bayana kwa kila mmoja wetu.

Haya sasa ndugu zangu Waislamu, tuamue ama kumfuata Bwana Mtume tupate salama au kutokumfuata na kuendeleza mila, tamaduni na ada zetu wenyewe tufikwe na msiba na adhabu kali iumizayo.

You can share this post!

Bandari yakamilisha ziara ya Afrika Kusini kwa kuizima...

AFCON 2019: Nigeria na Misri zafuzu mapema

adminleo