Makala

Mfumo wa elimu watatizika ahadi za Ruto zikifeli

Na  MERCY SIMIYU June 14th, 2025 Kusoma ni dakika: 2

MIAKA mitatu tangu Rais William Ruto aingie madarakani, sekta ya elimu ya juu nchini Kenya inakumbwa na mzozo mkubwa unaotishia ustawi wake.

Kati ya ahadi sita kuu alizotoa kuhusu elimu ya vyuo vikuu na vyuo vya kati katika kampeni yake ya uchaguzi mkuu wa 2022, ni moja tu iliyotekelezwa kikamilifu: kuidhinisha Open University of Kenya.

Ahadi tano zilizobaki — ikiwemo kuanzisha Baraza la Kitaifa la Ujuzi na Ufadhili litakalounganisha Bodi ya Mikopo ya Elimu ya Juu (HELB), TVET na Hazina ya Vyuo Vikuu; ujenzi wa vyuo vya TVET katika maeneo bunge 52; na kuanzisha mpango wa kitaifa wa mafunzo kwa wahitimu, bado hazijatekelezwa au zimekwama kutokana na changamoto za kisheria, kifedha au mipango.

Ahadi yenye utata zaidi ni kuhusu mfumo mpya wa ufadhili wa elimu ya juu ulioanzishwa miezi michache baada ya Rais Ruto kuapishwa. Mfumo huu uligawanya wanafunzi katika makundi matano ya uhitaji wa kifedha, kuanzia kundi la kwanza (wenye mahitaji makubwa zaidi) hadi kundi la tano (walio na mahitaji madogo zaidi na kutoa ufadhili kulingana na uhitaji.

Mfumo huu umekosolewa kwa kukosa uwazi na ushirikishaji katika hatua za kuundwa kwake. Rais aliteua kamati maalum kuupitia upya lakini ripoti yake haijatangazwa hadharani. Mahakama Kuu pia imesema unakiuka Katiba, jambo lililozua sintofahamu zaidi.Wakati huo huo, sekta ya elimu ya juu inakumbwa na nakisi kubwa ya kifedha.

Kulingana na Waziri wa Elimu Julius Ogamba, vyuo vikuu 23 vya umma vimetangazwa kufilisika. Kwa jumla vinadaiwa madeni ya jumla ya Sh72.2 bilioni huku Chuo Kikuu cha Nairobi kikiongoza kwa deni la zaidi ya Sh13 bilioni. Vyuo vingine vilivyo na madeni makubwa ni Kenyatta, Moi na Technical University of Kenya.Ukosefu wa fedha si tatizo pekee.

Mwanauchumi Dkt Samuel Nyandemo anasema usimamizi mbovu na uongozi dhaifu umechangia zaidi matatizo haya.Anapendekeza kupitiwa upya mfumo wa ufadhili, kushirikiana na sekta ya kibinafsi, na kurekebisha karo ili kuziba pengo la kifedha.Wakati huo huo, Bodi ya Mikopo ya Elimu ya Juu (HELB) pia inakabiliwa na mgogoro.

Bajeti yake ya sasa ya Sh41.1bilioni dhidi ya Sh76.3 bilioni zinazohitajika kufanikisha mfumo mpya wa ufadhili, na kuacha pengo la Sh35.1 bilioni.Mgogoro huu pia umelemaza shughuli za vyuo vikuu. Chuo Kikuu cha Moi kilifungwa kwa miezi mitatu kutokana na migomo ya wafanyakazi na kucheleweshwa kwa mishahara.

Serikali ililazimika kuingilia kati kwa kutoa Sh2.9 bilioni ili kurejesha hali ya kawaida. Hata hivyo, hatua kama hizi za dharura haziwezi kutatua matatizo ya kimsingi yaliyo katika mfumo.Mwezi Mei 2025, Mkuu wa Utumishi wa Umma Felix Koskei alitangaza marufuku ya miradi mipya katika vyuo 23 vilivyo katika hali ya kufilisika.

Ukaguzi wa kina wa kifedha unaendelea ili kubaini matumizi mabaya ya rasilmali.Waziri Ogamba, alipozungumza na kamati ya bunge mwezi Machi, alikiri kuwa hali ya hatari ya kifedha kwenye vyuo vikuu na kuhusisha changamoto hizo na kucheleweshwa kwa bajeti na uongozi mbovu.