Mhudumu wa M-PESA aliyetoweka apatikana akiwa amefariki
MWILI wa mhudumu wa M-Pesa Nakuru aliyetoweka kwa njia isiyoeleweka baada ya kuweka pesa katika benki umepatikana katika hifadhi ya maiti ya Nakuru city.
Hannah Waithera, 23, alitoweka Jumatano, Mei 21, baada ya kuondoka kazini katika barabara ya Kenyatta Avenue ndani ya Jiji la Nakuru, lakini akapatikana amefariki siku saba baadaye.
Bw Samuel Muiruri, mmoja wa jamaa wa familia ya mwathiriwa, alisema walipiga ripoti kuhusu kutoweka kwake katika kituo cha polisi cha Kaptembwa mnamo Aprili 28.
Alisema baada ya kusimulia kisa chao, afisa mmoja aliwafahamisha kwamba mwili wa mwanamke uliokuwa ukioza ulipatikana umetupwa katika shamba moja katika Kaunti-ndogo ya Nakuru Magharibi.
Afisa huyo aliiambia familia kuwa mwili huo ulipelekwa katika hifadhi ya maiti ya Nakuru City na kwamba wanapaswa kutembelea kituo hicho ili kuuona. Kwa mshangao, walipata kuwa mwili huo ulikuwa wa Waithera.
‘Tumekuwa tukitembelea vituo mbalimbali vya polisi na kuacha picha yake ili ibandikwe kila mahali. Hatukuwahi fikiria kuwa tutamkuta amefariki, tulikuwa na matumaini kuwa atarejea akiwa hai lakini ameaga,’ alisema.
Bw Muiruri alisema wakazi walitatizwa na harufu kali iliyokuwa ikitoka katika shamba hilo.Wakazi hao waliarifu uongozi ambao baadaye waliripoti kisa hicho kwa polisi.
‘Tumepelekwa Kituo Kikuu cha Polisi kwa maelezo zaidi, tangu ripoti ya awali ilipotolewa huko. Amelazwa katika chumba cha maiti kwa siku tatu zilizopita,’ alisema.
Jamaa mwingine Bi Ann Nduta alitoa wito kwa maafisa wa upelelezi kufanya uchunguzi wa haraka ili kubaini kilichomsababisha kifo chake.
Kulingana na Kamanda wa polisi wa Kaunti Ndogo ya Nakuru magharibi Stephen Kirui, walipata habari Jumatatu kutoka kwa mmoja wa wasimamizi wa shamba hilo kwamba walipata mwili uliokuwa ukioza.
Alisema maafisa wa Idara ya Upelelezi wa Makosa ya Jinai (DCI) na Huduma ya Kitaifa ya Polisi walifika eneo la tukio ambapo waligundua kuwa ni mwili wa mwanamke.
Bw Kirui alisema kuwa mwili huo ulikuwa umeharibika, na maafisa hao hawakuweza kubaini mara moja ikiwa ulikuwa na majeraha yoyote. Baadaye ilihamishwa hadi katika chumba cha kuhifadhia maiti kwa uchunguzi zaidi.Alibainisha kuwa uchunguzi ulibaini kuwa Bi Waithera aliuawa mahali pengine na mwili kutupwa humo.
“Tulikuwa tumemchukua alama za vidole ili zitusaidie kubaini lakini nimeambiwa kuwa familia imetambua maiti, wajitokeze watusaidie katika uchunguzi wetu, uchunguzi wa maiti utasaidia kujua chanzo cha kifo hicho,” alisema.