Makala

Mwanaharakati Agather aliyekamatwa pamoja na Bonface Mwangi, aachiliwa huru

Na WINNIE ONYANDO May 23rd, 2025 Kusoma ni dakika: 2

MWANAHARAKATI mwingine aliyekuwa akizuiliwa Tanzania ameachiliwa huru.

Agather Atuhaire ambaye pia ni wakili na mwanahabari alipatikana eneo la Mutukula kwenye mpaka wa Tanzania na Uganda.

Habari za kuachiliwa kwake zilisambazwa kwenye mtandao wa kijamii wa X na Godwin Toko ambaye pia ni naibu wa timu ya Agora.

“Hatimaye Agather ameachiliwa huru. Nimezungumza naye kupitia simu ya dadake. Aliachiliwa kwenye mpaka wa Uganda na Tanzania,” alisema Bw Toko.

Mwanaharakati huyo alikuwa akizuiliwa pamoja na Boniface Mwangi wa Kenya aliyeachiliwa huru jana.

Mwanaharakati huyo alikuwa hajulikani aliko kwa siku kadhaa baada ya kukamatwa wiki hii nchini Tanzania.

Boniface Mwangi alirejeshwa nchini kwa barabara Alhamisi kabla ya kupatikana akiwa ametupwa Ukunda, Kaunti ya Kilifi. Katika mkutano na waandishi wa habari, Mwangi alisema waliteswa pamoja na Agather, huku akitoa wito wa kuachiliwa kwake.

Mwanaharakati Hussein Khalid, Mkurugenzi Mtendaji wa VOCAL Africa, alithibitisha kuachiliwa kwa Agather, akisema kuwa hali yake si nzuri na akatoa wito wa haki kutendeka kwa wanaharakati hao.

 “Ameteswa, amejeruhiwa, mwili umevunjika lakini roho ni thabiti. Agather amepatikana. Lazima wawajibike kwa waliyomtendea Boniface Mwangi na Agather. Haki lazima itendeke na ionekane kutendeka,” alisema Khalid.

Agather na Mwangi walikamatwa jijini Dar es Salaam Mei 19 walipokuwa wakihudhuria kesi ya uhaini inayomkabili kiongozi wa upinzani nchini Tanzania, Tundu Lissu.

Familia ya Agather ilithibitisha kuwa alipatikana akiwa ametupwa eneo la mpakani  Mutukula usiku. Hali halisi ya kuachiliwa kwake haijafahamika wazi, na bado hajatoa tamko lolote kwa umma.

Kukamatwa kwao kuliibua hisia kali kimataifa, huku mashirika ya haki za binadamu yakitoa wito wa kuheshimiwa kwa haki za wanaharakati.

Mapema wiki hii, Rais Samia Suluhu alionya wanaharakati wa kigeni dhidi ya kuingilia mambo ya ndani ya Tanzania.

Hayo yalijiri muda mchache baada ya kiongozi wa chama cha People’s Liberation Party (PLP) Martha Karua kuwawasilisha malalamishi kwa Tume ya Umoja wa Afrika (AUC) kuhusu kile alichokitaja kama “kudorora kwa utawala wa sheria” nchini Tanzania.

Kwenye barua, aliyoiwasilishwa Alhamisi Mei 22, 2024 na  ambayo nakala yake alituma kwa makao makuu ya Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC) Bi Karua ametaja kuteswa kwa mwanaharakati Boniface Mwangi na wakili raia wa Uganda Agather Aruha kama kielelezo kukithiri mwenendo wa ukiukaji haki nchini Tanzania.

“Kuzuiliwa akwa Bw Mwangi na Bi Atuhiri kulitokea baada ya kuzuiliwa na  kufurushwa kwa raia sita wengine wa kigeni waliowasili katika uwanja wa Kimataifa wa Julius Nyerere kutaka kuhudhuria kikao cha mahakama kuhusu kesi inayomkabili kiongozi wa upinzani Tundu Lissu. Miongoni mwa waliozuliwa ni mimi na Jaji Mkuu wa zamani Willy Mutunga,” akaeleza Bi Karua ambaye ni Waziri wa zamani wa Haki na Masuala ya Kikatiba.

Mwanasiasa huyo, ambaye ni Wakili Mkuu, alisema kitendo hicho cha serikali ya Tanzania ni kinyume na viwango hitaji vya haki za kibinadamu nchini humo na kimataifa.

“Aidha, kitendo kama hicho kinashabihiana na mwenendo hatari wa utekaji nyara, mateso na mauaji ya kiholela yanayoendelea katika ukanda huu wa Afrika Mashariki,” akaongeza.

Bi Karua sasa anaitaka AUC kuingilia kati suala hilo na iilazimu Tanzania kukomesha vitendo vya ukiukaji wa haki inavyowatendea wakosoaji wake utawala wa Rais Samia Suluhu Hassan na wageni wanaodhaniwa kuwasawiri kuunga mkono upinzani nchini humo.