• Nairobi
  • Last Updated May 3rd, 2024 6:55 PM
NGILA: Sheria ya kupiga droni marufuku inaumiza Wakenya

NGILA: Sheria ya kupiga droni marufuku inaumiza Wakenya

Na FAUSTINE NGILA

NIKIPITIA video za mafuriko msimu huu wa mvua, nilimhurumia mno mwanamume mmoja anayeonekana kukwama katika ‘kisiwa’ kidogo katikati ya Mto Athi.

Kulingana na ripoti kwenye vyombo vya habari, mwanamume huyo kwa jina Vincent Musila alisalia katika eneo hilo ndogo la nchi kavu kwa siku tatu huku mvua ikiendelea kunyesha na maji ya mto yakiongezeka.

Hakuwa na namna yoyote ya kujiokoa, huku mamia ya wakazi wakitazama kwa umbali wasijue la kufanya kumuokoa au kumpa chakula au vazi lenye joto akisubiri kuokolewa.

Ingawa serikali hatimaye ilileta helikopta iliyombeba na kumuondolea dhiki hiyo, nilisalia kuishangaa kwa ilani ya kisheria mpya iliyobuni hapo Novemba 7.

Kulingana na Mamlaka ya Usafiri wa Angani (KCAA), kwa sasa ni hatia kwa mtu yeyote kuendesha droni za kisasa katika anga ya Kenya, iwe kwa manufaa ya filamu, usalama au uokoaji.

Ilani hiyo inaeleza kuwa yeyote atakayenaswa akifanya hivyo atasukumwa ndani mwaka mmoja au kupigwa faini ya Sh100,00, au adhabu zote mbili.

Lakini nikizungumza na mkuu wa kampuni ya droni, simu na mtandao wa 5G, Nokia Bw John Harrington, niling’amua kuwa droni zimekuwa zikitumika katika mji wa Sendai, nchini Japan kuwaokoa watu wakati wa majanga ya tsunami na mafuriko, jambo ambalo limesaidia kuokoa maelfu ya watu.

Droni hutumiwa kuwapelekea watu waliokwama vyakula, maji na nguo, huku pia zikiwaondoa kutoka maeneo ya hatari na kuwapeleka maeneo salama kupitia mawasiliano ya teknolojia ya mawimbi ya 4G LTE.

Hapa Kenya, tumeshuhudia sera hasi ambazo badala ya kusaidia wananchi wakati wa majanga, zinachangia katika kuwadunisha zaidi.

Iweje serikali ipige marufuku ubunifu katika matumizi ya droni, licha ya kujionea watu wengi wakiathirika na hata kufariki wakati huu wa mvua?

Vipi isitambue umuhimu wa teknolojia katika kuwahamisha wakazi walio katika maeneo ya mafuriko na kuwapa chakula?

Na si mafuriko tu, maporomoko ya ardhi yamechangia watu wengi kupoteza makazi yao na kulala kwenye baridi usiku kucha huku wakinyeshewa wasipate msaada.

Ni wakati wa kuwa na utu kwa binadamu wenzetu. Teknolojia ambayo ingemsaidia Bw Musila kufika kwake nyumbani inafaa kurejeshwa.

Haifai kwa KCAA kupiga droni marufuku kwa kuwa serikali imekuwa inatuhadaa inaposema imejitayarisha kukabiliana na majanga haya.

Kusubiri siku tatu kisha uchukue hatua hakutaokoa watu wengi. Tunahitaji droni ziwepo ili tukuze ubunifu wetu katika matumizi yake, mojawapo ikiwa ni suluhu kwa kuokoa au kuwatumia vyakula waathiriwa wa majanga walio maeneo ya mbali yasiyofikika na binadamu.

You can share this post!

NGILA: Teknolojia itumiwe kuwapa tumaini watoto wa wakimbizi

NGILA: Sharti sote tuheshimu sheria ya kulinda data

adminleo