Pambo

Faida za kucheza na kufanya mambo ya mzaha na watoto

Na BENSON MATHEKA June 2nd, 2025 Kusoma ni dakika: 2

IWAPO wewe ni mzazi wa mtoto mchanga au wa umri wa chekechea, tayari unajua kuwa utani wa kipuuzi na michezo ya kuigiza vinaweza kuleta furaha katika siku ulizo na shughuli nyingi.

Lakini kwa mujibu wa utafiti mpya, kufanya mzaha na kuigiza si tu burudani—vinaweza kuwa muhimu sana kwa ukuaji wa mtoto.

Katika mradi uliodhaminiwa na Baraza la Utafiti wa Kiuchumi na Kijamii (ESRC), watafiti wa Chuo Kikuu cha Stirling nchini Uingereza, walichunguza iwapo watoto wadogo wanaweza kuelewa dhana za mzaha na kuigiza.

Waligundua kuwa watoto wadogo wa kuanzia umri wa miezi 15 wanaweza kuelewa na kufurahia dhana hizi. Zaidi ya hayo, walibaini kuwa kujua jinsi ya kushiriki mzaha na kuigiza kunaweza kuwasaidia watoto kukuza ujuzi muhimu katika maisha wanapokua.Mzaha na michezo ya kuigiza huambatana na faida nyingi.

Watoto wanapojihusisha na michezo ya kuigiza na kujaribu majukumu tofauti, huwa wanaendeleza ubunifu wao, uwezo wa kutatua matatizo, na kuelewa ulimwengu unaowazunguka.

Wakati wanapojifunza kushiriki mzaha kwa njia inayoeleweka na ifaayo, wana uwezo mkubwa wa kudhibiti msongo wa mawazo, kupata marafiki na kuelewana vizuri na wengine.

Ingawa kucheza na watoto kwa njia ya mzaha na kuigiza ni muhimu, mzazi mwenye shughuli nyingi anaweza kukosa muda wa kufanya hivyo.

Hata hivyo, watafiti wanawahimiza wazazi kutenga muda kila siku kuweka kando mambo mazito na kufurahia kuwa wapuuzi, wabunifu na watoto wao.

“Ingawa vipindi vya watoto vya kuchekesha vinapatikana kwa wingi katika runinga, muda wa kuwa na mzazi ni muhimu zaidi kuliko kutulia na kutazama runinga,” asema mtaalamu wa malezi dijitali Susan Kimani.

Anasema njia moja ya kuongeza muda wa kucheza ni kutenga muda wa mapumziko na starehe. Ni rahisi kufurahia kuwa pamoja na mtoto wako bila presha ya kukimbizana na saa kwa sababu ya shughuli.

“Njia bora ya kufunza watoto kucheza michezo ya kuigiza ni kuwapatia vifaa vya kuchochea ubunifu wao. Unda eneo la kuvaa mavazi na mtoe nguo mbalimbali pamoja na vitu vingine salama kwa matumizi ya watoto. Pia weka vifaa vya sanaa vinavyofaa kwa umri wao kama vile rangi za kuchora na mcheze pamoja nao,” aeleza.

Wakati mwingine mtoto atakuwa na hamu ya kucheza na wakati mwingine hatakuwa tayari. Fuata mwongozo wake na tafuteni hali zinazowafaa nyote wawili.

Kwa hivyo, kufanya mzaha na kuigiza si upuuzi tu, ni njia muhimu ya kukuza maendeleo ya kijamii, kihisia na kiakili ya watoto.

Ukichukua muda wa kucheka na kuigiza na mtoto wako, unamwezesha kukuza ujuzi wa maisha atakaohitaji kwa maisha yote.