Akili MaliMakala

Sekta ya kahawa imekabiliwa na changamoto – ripoti ya KNCCI

Na SAMMY WAWERU March 15th, 2026 Kusoma ni dakika: 3

SEKTA ya kahawa nchini Kenya, ambayo kwa muda mrefu imejulikana kwa maharagwe yake maalum ya Arabica yenye ubora wa hali ya juu, sasa inakabiliwa na changamoto kubwa za haki za kibinadamu, utawala mbovu na uendelevu hafifu, zinazotishia ukuaji wake.

Haya yamebainishwa katika ripoti mpya iliyotolewa na Kenya National Chamber of Commerce and Industry (KNCCI).

Kwenye ripoti hiyo, inayojulikana kama Sector-Wide Impact Assessment (SWIA), KNCCI ilichapisha tathmini ya sekta hii pana ikiainisha changamoto hizo.

Tathmini hiyo inaangazia hali ya ajira, athari za mazingira na utekelezaji wa mbinu endelevu.

Inaelezea kwa kina hatari za ukiukaji wa haki za binadamu katika uzalishaji wa kahawa na kuchunguza namna wanunuzi wa kimataifa wanavyotekeleza wajibu wa kuchunguza na kushughulikia masuala hayo wanaponunua kahawa kutoka kwa wakulima.

“Kwa muda mrefu tulikuwa tumetabiri hali hii, na matokeo ya tathmini yamethibitisha kuwepo kwa changamoto nyingi za haki za binadamu katika ngazi zote za uzalishaji wa kahawa,” alisema Dkt Erick Rutto, Rais wa KNCCI wakati wa uzinduzi wa ripoti hiyo Jijini Nairobi.

Katika ngazi ya wakulima wadogo – yaani wale wa mashamba madogo, ripoti hiyo imebaini kuwa ajira za vibarua, ambazo mara nyingi zinahusisha wanawake, huwaweka wafanyakazi katika mazingira hatari.

Changamoto wanazopitia ni pamoja na ukosefu wa vifaa maalum vya kujikinga wanapopulizia dawa kwa mikahawa na kahawa yenyewe, na malipo duni – ripoti ya KNCCI ikiyataja kuwa ya kiwango cha chini cha mshahara kinachotakiwa kisheria.

Mkulima akikagua kahawa kwenye shamba lake Kaunti ya Nyeri. Picha|Sammy Waweru

Dkt Rutto anasema kuwa wakulima wadogo pia wanakabiliwa na gharama kubwa za pembejeo, upatikanaji wa miche ya kahawa inayostahimili athari za tabianchi hasa ukame, kiangazi, na magonjwa, pamoja na ukosefu wa maarifa ya mbinu bora za kilimo endelevu.

Utafiti huo ulifanywa na KNCCI kwa ushirikiano na Danish Institute for Human Rights (DIHR) pamoja na Kenya National Commission on Human Rights (KNCHR), kwa ufadhili wa Swedish International Development Cooperation Agency (Sida).

Mahojiano na wanunuzi na wafanyabiashara wa kahawa yalibaini kuwa wengi wao hutegemea vyeti vya kimataifa kama vile Rainforest Alliance, Fairtrade International, C.A.F.E. Practices na 4C Association ili kudhibiti hatari za ukiukaji wa haki za kibinadamu.

Hata hivyo, tathmini hiyo imeonyesha kuwa ukaguzi wa vyeti hivyo mara nyingi haufiki katika ngazi ya mkulima mdogo kwa sababu stakabadhi hizo hushikiliwa na vyama vya ushirika.

Kwa sababu hiyo, faida zinazotokana na vyeti hivyo—hasa malipo ya ziada, hazifikii wakulima na wafanyakazi.

Hali hii imesababisha pengo kubwa kati ya mifumo ya vyeti na hali halisi mashambani.

“Tathmini imeonyesha wazi kwamba ingawa wanunuzi wa kimataifa wanafanya uchunguzi wao wa haki za kibinadamu, vyeti pekee haviwezi kuchukua nafasi ya ushirikiano wa moja kwa moja na wazalishaji ili kushughulikia hatari zinazowakodolea macho,” alisema Dirk Hoffmann, mshauri mkuu katika DIHR.

Utafiti wa shambani ulifanyika katika kaunti za Kirinyaga, Nyeri, Kiambu, Embu, Kericho na Nandi, kati ya robo ya mwisho wa mwaka 2024 na robo ya kwanza yam waka uliopita, 2025.

Watafiti walitumia mbinu mbalimbali ikiwa ni pamoja na uchambuzi wa nyaraka, mahojiano, majadiliano ya vikundi na uchunguzi wa moja kwa moja katika mtandao mzima wa sekta ya kahawa.

Mti wenye kahawa tayari kuvunwa. Picha|Sammy Waweru

Kulingana na Afisa Mkuu Mtendaji wa KNCCI, KK Mutai, matokeo ya utafiti huo ni muhimu hasa wakati huu ambapo Kenya inaendelea kutekeleza mageuzi katika sekta ya kahawa huku masoko ya kimataifa yakisisitiza uwajibikaji katika biashara na kuheshimu haki za kibinadamu.

Aidha, utafiti huo umefanyika wakati uzalishaji wa kahawa nchini umeendelea kusalia chini ya magunia milioni moja ya kilo 60 kila mwaka licha ya mahitaji makubwa katika soko la kimataifa.

Hali hiyo imechangiwa na mashamba ya kahawa kugeuzwa kuwa miradi mingine ya kibiashara na maendeleo kama vile ujenzi wa nyumba na makazi.

Kwa mujibu wa tathmini ya KNCCI, miti ya kahawa iliyozeeka, mikurupuko ya magonjwa, matumizi ya kiwango cha chini cha mbinu za kisasa kwenye kilimo na mabadiliko ya tabianchi vinaendelea kudhoofisha uzalishaji.

Sekta ya kahawa nchini Kenya inatawaliwa na zaidi ya wakulima wadogo 800,000 wanaochangia takribani asilimia 99.6 ya wazalishaji wote, pamoja na karibu mashamba makubwa 3,000 yaliyosambaa katika kaunti 33.

Kanda za kati na magharibi mwa Kenya, ndizo zinazoongoza katika uzalishaji wa kahawa.

Ripoti ya KNCCI inatoa mapendekezo kwa serikali, wanunuzi wa kimataifa, vyama vya ushirika na wadau wengine kwenye mtandao pana wa sekta ya kahawa kuimarisha uwajibikaji wa kibiashara na kuhakikisha kuna mazingira bora kuleta ushindani.